Gor Mahia yaondoka na jeshi la watu 18 kuikabili Yanga

Muktasari:

Mabingwa hao wa Kenya wanakamata nafasi ya pili  katika Kundi D

Nairobi. Mabingwa wa soka nchini, Gor Mahia wameondoka nchini, kuelekea nchini Tanzania kuikabili Yanga SC, katika mechi ya marudiano ya Kundi D, Kombe la Shirikisho la Afrika, itakayopigwa kesho kwenye Uwanja wa Taifa, Jijini Dar es  Salaam, kuanzia saa 10 alasiri.

Kwa mujibu wa mtandao wa klabu hiyo, kikosi cha wachezaji 18 pamoja na viongozi saba wakiongozwa na Mwenyekiti wao Ambrose Rachier, waliondoka jana usiku majira ya saa tano, ambapo siku ya leo watafanya mazoezi mepesi kabla ya kuwakabili Yanga kesho, Jumapili, Julai 29.

Gor Mahia, wanaoongoza msimamo wa ligi ya Kenya, wakiwa hawajapoteza mchezo hata mmoja, wataingia katika mechi ya kesho, wakiwa na morali ya hali ya juu, hasa baada ya kuwatwanga mashemeji zao AFC Leopards 2-1 na baadae kuisasambua Posta Rangers 3-1, huku pia ikikumbukwa kuwa katika mechi ya kwanza, iliyopigwa Kasarani waliitandoka Yanga 4-0.

Kikosi cha Dylan Kerr kimepata morali baada ya kurejea kwa beki wake, asiye na masihara Joash Onyango kama ilivyo kwa Yanga ambayo inajivunia kurejea kwa Kelvin Yondani. Lawrence Juma, Bernard Ondiek, Cercidy Okeyo, Samuel Onyango, Kevin Omondi, Charles Momanyi and Shaban Odhoji pia wamesafiri na timu.

Kogalo wanashika nafasi ya pili kwenye msimamo wa kundi D, wakiwa na pointi tano, pointi mbili ya vinara wa kundi USM Algiers, wenye pointi saba. Yanga wanavuta mkia kundini wakiwa na pointi moja tu.

Kikosi kamili kilichoenda Tanzania:

1.Boniface Oluoch 2. Shaaban Odhoji 3. Charles Momanyi 4. Joash Onyango 5. Haron Shakava 6. Godfrey Walusimbi 7. Philemon Otieno 8. Humphrey Mieno 9. Cercidy Okeyo 10. Boniface Omondi 11. Samuel Onyango 12. Francis Kahata 13. Lawrence Juma 14. Kevin Omondi 15. Jacques Tuyisenge 16. Ephrem Guikan 17. Bernard Ondiek 18. George Odhiambo

Benchi la Ufundi: Dyllan Kerr, Zedekiah Otieno, Jolawi Obondo, Patrick Opiyo, Willis Ochieng, Fred Otieno, George Omondi.