Ujeuri wamponza Diego Costa

Muktasari:

Atletico Madrid yamuanzishia mazoezi maalumu ili kupunguza uzito kwa ajili ya kumuweka fiti kama awali.

Madrid, Hispania. Diego Costa ameanza maisha mapya katika klabu yake ya zamani Atletico Madrid inayoshiriki Ligi Kuu Hispania.
Costa alirejea kwa mbinde Atletico Madrid, baada ya kocha wa Chelsea Antonio Costa kumwambia hamtaki katika kikosi chake muda mfupi baada ya kutua Stamford Bridge.
Mchezaji huyo mzaliwa wa Brazil mwenye uraia wa Hispania, aligoma kurejea Chelsea licha ya kukingiwa kifua na vigogo wa klabu hiyo kabla ya kupigwa bei katika usajili wa majira ya kiangazi.
Costa, 29, juzi alikuwa na uso wa tabasamu alipokuwa akijifua katika mazoezi na wachezaji wenzake kwa lengo la kujiweka fiti.
Pia mshambuliaji huyo alipewa mazoezi binafsi ili kurejesha 'shepu' yake ya kawaida baada ya kubainika ana uzito mkubwa.
Baadhi ya wachezaji wa timu hiyo waliokuwa wakipasha moto misuli ni Fernando Torres, Kevin Gameiro na Angel Correa.
Mshambuliaji anataka kujiweka fiti kuendeleza makali katika kikosi hicho kama alivyokuwa Chelsea alipokuwa kinara wa mabao licha ya kutajwa kuwa ni mtukutu.
Baada ya kurejea Atletico kwa 57 pauni milioni, klabu hiyo itasubiri kuanza kupata huduma yake hadi mwakani kwa kuwa imefungiwa kusajili majira ya kiangazi baada ya kukiuka kanuni.