Chirwa afunguka mazito Yanga na Simba

Muktasari:

  • Pia, amesema kwa mchezaji kucheza Simba au Yanga, ni lazima awe tayari kubeba lawama ikiwemo kuzomewa na mashabiki ambao siku zote wamekuwa wakitaka kumuona mchezaji anafanya vizuri hasa kufunga mabao tu.

MSHAMBULIAJI aliyeondoka Yanga, Obrey Chirwa, amempa ushauri wa bure straika mpya wa Simba, Adam Salamba, asikimbilie kupiga penalti akimuomba awaachie wakongwe wa timu kazi hiyo.

Pia, amesema kwa mchezaji kucheza Simba au Yanga, ni lazima awe tayari kubeba lawama ikiwemo kuzomewa na mashabiki ambao siku zote wamekuwa wakitaka kumuona mchezaji anafanya vizuri hasa kufunga mabao tu.

Ushauri wa Chirwa umekuja siku chache baada ya Salamba kupoteza penalti katika mchezo wa kirafiki dhidi ya Asante Kotoko ya Ghana wa kuadhimisha Tamasha la Simba Day uliochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Jumatano na kumalizika kwa sare ya bao 1-1.

Salamba alipewa penalti hiyo dakika ya 86, lakini wakati akitegemewa kufunga, alipiga kiki dhaifu ambayo iliishia mikononi mwa kipa wa Kotoko.

Akizungumza katika mtandao wa Instagram, Chirwa, alisema timu za Simba na Yanga zinampenda mchezaji anapofunga tu na zinamhukumu kwa kosa moja tu, hivyo ili mchezaji aweze kulinda kipaji chake anatakiwa kuachana na masuala ya upigaji penalti.

Alisema Salamba ni chipukizi pale Simba ambapo kuna wakongwe kama Emmanuel Okwi wanaotakiwa kuachiwa wao masuala ya penalti kwani wameshajijenga tofauti na yeye.

“Salamba ni mdogo wangu, naomba nimshauri kuwa aachane na suala la upigaji penalti kwani timu anayocheza ina wakongwe wengi ambao wanaweza kufanya hivyo, kwa upande wake anatakiwa kuwa makini kujiimarisha zaidi katika uchezaji, mambo mengine awaachie wakongwe,” alisema.

“Ukitaka kuonyesha una uwezo sana katika timu hizo mbili (Simba na Yanga) basi usiwe na makosa madogo madogo ya kimchezo kwa sababu zina mashabiki ambao muda wote wanataka matokeo mazuri tu na si vinginevyo.”

Chirwa aliongeza kuwa soka ni mchezo wa makosa, hivyo mashabiki wanatakiwa kutambua hilo. Pia alitumia nafasi hiyo kuwaomba mashabiki kuachana na tabia za kuwahukumu wachezaji kwa sababu wanawatoa katika mchezo suala ambalo linachangia kuwashusha viwango.

“Hakuna kitu kibaya kama kuchukiwa na shabiki hasa wa timu hizo mbili kwa sababu lazima mchezaji utatoka mchezoni, hata ukipoteza pasi kwa bahati mbaya unazomewa, ni changamoto sana,” alisema.

“Jambo mashabiki wanapaswa kuliangalia kivingine.”