Carragher: Rashford ondoka Manchester United

Muktasari:

Carragher ametoa ushauri huo baada ya Rashford mwenye miaka 20 kuifungia nchi yake bao pekee katika ushindi wa 1-0 dhidi ya Uswisi katika mechi ya kirafiki iliyochezwa jana Jumanne mjini Leicester, England.

Leicester, England. Mlinzi wa zamani wa Liverpool, Jamie Carragher, amemtaka mshambuliaji kinda wa England, Marcus Rashford kuondoka Manchester United ikiwa anataka kulinda na kukiendeleza kipaji chake.

Carragher ametoa ushauri huo baada ya Rashford mwenye miaka 20 kuifungia nchi yake bao pekee katika ushindi wa 1-0 dhidi ya Uswisi katika mechi ya kirafiki iliyochezwa jana Jumanne mjini Leicester, England.

Mshambuliaji huyo chipukizi, pia aliifungia England bao la kufutia machozi walipofungwa mabao 2-1 na Hispania katika mchezo wa ‘Euro Nations League’ uliochezwa Jumamosi iliyopita kwenye dimba la Wembley mjini London.

Kutokana na hilo Carragher alisema, ili kuboresha kiwango chake ni lazima Rashford aondoke klabu hiyo yenye maskani yake Old Trafford na kutafuta timu ambako atakuwa na uhakika wa kucheza kila mechi katika nafasi yake ya ushambuliaji wa kati.

“Kwa sasa mshambuliaji chaguo la kwanza kwa Jose Mourinho kwa ushambuliaji pale Manchester ni Romelu Lukaku na anastahili kwa kazi nzuri anayoifanya uwanjani hivyo Rashford ni lazima aondoke kwa sasa,” alisema Carragher.

Mlinzi huyo wa zamani alikumbushia jinsi Lukaku alivyojiongeza na kuondoka Chelsea baada ya kuona hana nafasi ya kuanza uamuzi uliomfaa kwani alipojiunga na Everton alikuwa na uhakika wa namba jambo lililokiboresha kiwango chake baada ya muda mfupi na kuanza kupapatikiwa na timu mbali mbali.

“Nadhani Rashford anaweza kwenda klabu kama Everton ambako atakuwa na uhakika wa kucheza kila wiki jambo litakalokiboresha kiwango chake tofauti na sasa ambapo analazimika kusubiri benchi,” alisema.