Bocco awaliza Prisons mapema

Muktasari:

Bocco sasa amefikisha mabao 13,

Dar es Salaam. Mshambuliaji John Bocco ameifanya Simba kwenda mapumziko wakiwa mbele kwa bao 1-0 dhidi ya Prisons kwenye mchezo Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Bocco alifunga bao hilo la kuongoza kwa Simba dakika 35, akiunganisha kwa kichwa mpira wa krosi ya Erasto Nyoni aliopiga na kugonga mwamba na kumkuta nyota huyo aliyepiga mbizi kufunga.

Bocco sasa amefikisha mabao 13, katika orodha ya wafungaji inayoongozwa na Emmanuel Okwi mwenye magoli 18 hadi sasa.

Mchezo huo unashudiwa na mashabiki wachache pamoja na mvua kuacha kunyesha lakini majukwaa mengi ya uwanja huu viti vyake ni vyeupe.

Simba wamevaa jezi nyekundu na bukta nyeupe huku soksi zikiwa za rangi nyekundu wakati wageni Prisons wamevaa jezi za rangi ya kijani.

Mwamuzi Shomary Lawi kutoka Kigoma ndiye atakayechezesha mechi ya leo akisaidiwa na washika vibendera Gasper Ketto kutoka Morogoro na Kassim Safisha wa Pwani wakati refa wa mezani ni Abdallah Selega wa Dar es Salaam. Kamishna wa mchezo wa leo ni Charles Mchau kutoka Kilimanjaro.

Matokeo ya michezo mingine inayoendelea Ndanda imechapwa mabao 3-1 na Ruvu Shooting nayo Kagera Sugar imefungwa bao 1-0 na Mtibwa Sugar mechi zote ni mapumziko.


Vikosi

Simba: Aishi Manula, Shomari Kapombe, Mohammed Hussein, Yusuph Mlipili, Murushid Juuko, Erasto Nyoni, Shiza Kichuya, Jonas Mkude, John Bocco, Emmanuel Okwi, Asante Kwasi

Prisons: Aron Kalambo, Benjamin Asukile, Leons Mutalemwa, Nurdin Chona, James Mwasote, Jumanne Elfadhil, Salum Kimenya, Cleophace Mukandala, Mohammed Rashid, Freddy Chudu,Eliuter Mpepo