Binslum ataka umoja Coastal Union
Muktasari:
- Wagosi ya kaya wametambulisha jezi zao mpya jana Jumapili kwa kucheza mechi ya kirafiki dhidi ya Arusha United na kushinda bao 1-0 ikiwa ni maandalizi kuelekea katika mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya African Lyon utakaochezwa, Septemba 14 jijini Dar es Salaam.
Tanga. Mashabiki wa Coastal Union wametakiwa kuiunga mkono timu hiyo ili kuendelea kufanya vizuri katika Ligi Kuu Bara msimu huu.
Wagosi ya kaya wametambulisha jezi zao mpya jana Jumapili kwa kucheza mechi ya kirafiki dhidi ya Arusha United na kushinda bao 1-0 ikiwa ni maandalizi kuelekea katika mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya African Lyon utakaochezwa, Septemba 14 jijini Dar es Salaam.
Coastal Union inapointi tano mkononi baada ya kucheza mechi tatu kwenye uwanja wa wake wa nyumbani wa Mkwakwani dhidi ya Lipuli FC, Biashara United pamoja na KMC FC.
Mdhamini wa timu hiyo, Nassor Binslum alisema wanachama na mashabiki wa Coastal Union wanatakiwa kutambua timu yetu imejaza wachezaji vijana wengi kwa hiyo kunaitajika uvumilivu.
Binslum alisema kadri siku zinavyozidi kwenda timu yetu inazidi kubadilika kwa sababu ukingalia walivyocheza dhidi ya Lipuli FC ni tofauti kabisa na KMC FC na hata kwenye mchezo wa kirafi dhidi ya Arusha United.
"Wadau wa michezo jijini hapa wanatakiwa kuwa wavumilivu kwa kipindi hiki kifupi kwa sababu muda si mrefu timu itakaa vizuri na kucheza katika kiwango bora kabisa," alisema Binslum.
Aliwaomba mashabiki na wanachama wa Coastal Union kuendeleza umoja uliyopo sasa ili kutowapa nafasi wabaya wao.