Neymar, Mbappe kuonekana king’amuzi cha StarTimes

Kampuni ya Star Media (T) Ltd kupitia king’amuzi chake cha StarTimes imetangaza kurejea kwa ligi kuu ya Ufaransa maarufu kama Ligue 1 kwa msimu wa 2018/19. Taarifa hiyo ilitolewa na Meneja Mahusiano wa Kampuni hiyo, Juma Suluhu katika mkutano na waandishi wa habari.

Ligi kuu ya nchini Ufaransa imekuwa ikionyeshwa kupitia king’amuzi hicho kwa takribani misimu minne sasa na kwa mara nyingine tena StarTimes wamepata kibali cha kuonyesha ligi hiyo ambayo ni chimbuko la wachezaji wengi wenye vipaji waliowika katika soka na wanaoemdelea kutamba katika medani za soka, miongoni mwao ni mkongwe Didier Drogba aliyewahi kucheza ligi hiyo na Eden Hazard aliyecheza klabu ya Lille. Kwa sasa wanaotamba katika ligi hiyo ni kinda wa kimataifa wa Ufaransa Kylian Mbappe na nyota wa Brazil Neymar Jr Santos ambao wote wanakipiga katika klabu ya PSG ya jijini Paris.

“Katika msimu huu mpya wa Ligue 1, wateja wetu wanapata nafasi ya kipekee kabisa kutazama wachezaji walioweza kufanya vizuri katika Kombe la Dunia wakiwa na timu zao za taifa kama vile Mbappe, Neymar na Radamel Falcao. Wateja wetu wataitazama ligi hii kwa kulipia kifurushi cha MAMBO upande wa Antenna kwa Tsh 13,000 tu kwa mwezi na kifurushi cha SMART kwa watumiaji wa Dish Tsh 19,000 tu kwa mwezi”. Bw. Juma Suluhu, Meneja Mahusiano Star Media (T) Ltd.

Ligue 1 imeongezeka umaarufu zaidi na kuwa kivutio kwa watazamaji na wanasoka bora kwenda kucheza katika ligi hiyo miaka ya hivi karibuni, hivyo kuongeza ushindani miongoni mwa timu zinazoshiriki katika ligi hiyo. Mabingwa wa msimu uliopita, klabu ya PSG wanapewa nafasi kubwa ya kutetea ubingwa wao kutokana na uwezo na ubora wa wachezaji wake, lakini hii si kubeza uwezo na viwango vya timu zilizobaki.

Mwaka jana timu kama Olympic Lyon ilionyesha uwezo mzuri kwenye ligi, wachezaji wa kiwango cha juu kama Mempis Depay, Bertrand Traore na Nabil Fekir pia katika kikosi cha Marseille kuna wachezaji wenye ubora kama Florian Thauvan na Dimitri Payet bila kuwasahau Monaco ambao walishika nafasi ya pili msimu uliopita wakiongozwa na nahodha wao mkongwe Radamel Falcao, kinda wa ubelgiji Youri Tielemans na wengine wengi.

“Baada ya Kombe la Dunia mmekuwa mkijiuliza ni nini kinafuata, tulianza na ICC ambayo ilizikutanisha timu za Mabingwa wa muda wote na sasa Msimu wa Ligue 1 ndo huo unaanza Mubashara ndani ya king’amuzi chenu pendwa, wiki mbili zijazo Bundesliga pia itarejea. Tunakwambia na Baki na Sisi Soka limenoga,” aliongeza Juma Suluhu.

Ligue 1 inaanza kutimua vumbi ijumaa saa 3:45 Usiku kwa kuwakutanisha Olympic Marseille na Toulouse, mchezo ambao utakuwa mubashara kupitia chaneli ya World Football ndani ya king’amuzi cha StarTimes.