HABARI MPYA: Ukweli wa Dismas Ten kujiuzulu Yanga huu hapa

BAADA ya Taarifa kusambaa kwamba Ofisa Habari wa Yanga, Dismas Ten ameandika barua ya kujiuluzu nafasi yake ndani ya timu hiyo, kiongozi huyo ameibuka na kukanusha habari hizo zinazosambaa kwenye mitandao ya kijamii.

Ten aliliambia Mwanaspoti leo Ijumaa kwamba hajafikilia kuiacha Yanga katika kipindi hiki kwani ni kipindi kigumu ambacho timu yake inapitia na kila mmoja anatambua.

“Siwezi kuiacha timu yangu kipindi hiki ambacho ni kigumu sana kwetu, sijaandika barua popote bado naendelea na kazi yangu kwa sababu mimi ni mwajiriwa wa Yanga,” alisema.

Ten aliongeza kwamba hizo ni habari zinazosambazwa na watu ambao wanataka kuivuruga Yanga, kwani yeye bado ni mwajiriwa wa Yanga.

Awali, tangu usiku wa leo Ijumaa kulikuwa na taarifa kuwa ofisa huyo habari wa Yanga, Ten naye aamua kujiuzulu nafasi yake.

Taarifa iliyokuwa ikisambaa mitandaoni ilieleza kwamba Ten ameandika barua kwenda kwa makamu mwenyekiti  wa klabu hiyo akidai ameamua kujiuzulu kutokana matatizo ya afya yake.

Hata hivyo ameweka wazi kwamba watau wanaosambaza taarifa hizo wana lengo la kumchafua na mashabiki wa Yanga wazipuuze.