#WC2018: Luca Modric ndio mchezaji bora wa Kombe la Dunia 2018

Nahodha wa Croatia, Luka Modric

Muktasari:

Kiungo huyo wa Real Madrid, ameshinda tuzo hiyo akiwabwaga Kylian Mbappe, Antoine Griezmann na nahodha wa Ubelgiji Eden Hazard ambao walikuwa wanapigiwa upatu kuibuka washindi hasa baada ya kuonesha kiwango kilichotukuka katika michuano hiyo iliyofika tamati rasmi leo, Jumapili, Julai 15, 2018.

Moscow, Russia. Licha ya kushuhudia timu yake ikishindwa kutwaa ubingwa wa Kombe la Dunia, nahodha wa Croatia, Luka Modric ameshinda tuzo ya mchezaji bora wa mashindano.

Kiungo huyo wa Real Madrid, ameshinda tuzo hiyo akiwabwaga Kylian Mbappe, Antoine Griezmann na nahodha wa Ubelgiji Eden Hazard ambao walikuwa wanapigiwa upatu kuibuka washindi hasa baada ya kuonesha kiwango kilichotukuka katika michuano hiyo iliyofika tamati rasmi leo, Jumapili, Julai 15, 2018.

Croatia walifungwa mabao 4-2 na Ufaransa katika mchezo mkai wa fainali uliopigwa katika dimba la Luzhniki ambao ni uwanja wa taifa wa urusi. Mabao ya Ufaransa yaliwekwa kambani na Mario Mandzukic (alijifunga), Antoine Griezmann, Kylian Mbappe na Paul Pogba huku Croatia wao wakijipatia mabao yao kupitia kwa Mario Mandzukic na Iva Perisic.

Wachezaji wengine ambao wamewahi kubeba tuzo hiyo ni pamoja na Lionel Messi, Zinedine Zidane, Ronaldo de Lima, Davor Suker, Diego Maradona na Paolo Rossi. Tuzo hii, inamuweka Modric katika nafasi nzuri ya kushinda tuzo ya mwaka huu ya Ballon d'Or.