Kenya yatamba mashindano Kanda ya Tano

Muktasari:

  • Tanzania ndio ilinyakua medali nyingi lakini ilizidiwa medali za dhahabu na Kenya na kufanya kuenguliwa kileleni kama ilivyokuwa mwaka uliopita Tanzania ilipozidiwa medali moja ya dhahabu na Wakenya.

Arusha. Wanariadha wa Kenya wameendelea kufanya vyema katika mashindano ya vijana ya Kanda ya Tano yaliyofanyika mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam kwa kubeba medali nyingi za dhahabu na kuwaengua wenyeji kileleni.
Tanzania ndio ilinyakua medali nyingi lakini ilizidiwa medali za dhahabu na Kenya na kufanya kuenguliwa kileleni kama ilivyokuwa mwaka uliopita Tanzania ilipozidiwa medali moja ya dhahabu na Wakenya.
Tanzania imevuna medali 13, dhahabu 4, fedha 5 na shaba 4, wakati Kenya imevuna 12, dhahabu 8, fedha 2 na shaba 2,Sudani imemaliza nafasi ya tatu ikinyakua medali sita, dhahabu tatu, fedha mbili na shaba moja, Uganda wakimaliza wa nne, ikiondoka na medali tatu, dhahabu moja, fedha mbili.
Wawakilishi kutoka Eritrea wakimaliza wa tano na medali tano, fedha tatu na shaba mbili, huku Zanibar wakimaliza nafasi ya sita wakiwa na Medal, fedha moja na shaba tano, Djibout wakimaliza wa saba na medali tatu, fedha moja na shaba mbili na Somalia wakiondoka patupu.
Kenya imeendelea kutamba katika mashindano hayo ikiwa ni mara ya tatu mfululizo, licha ya mwaka jana Tanzania kwa na medali nyingi lakini ilishushwa na Kenya kutokana na kuwa na medali nyingi za dhahabu.
 
Katibu Mkuu wa RT Wilhelm Gidabuday alisema ni mafanikio makubwa wameyapata kutokana na mfumo wa kuwatumia wanafunzi waliowapata kutoka kwenye michezo ya shule (Umisseta).
“Kurudi kwa michezo shuleni inafungua fulsa nyingine kwa vijana wenye vipaji kwani bila hivyo tungeendelea na mfumo wetu wa kusaka wawakilishi kupitia vyama vya mikoa njia ambayo sio nzuri kama hii ya kupitia Umisseta,” alisema Gidabuday.
Aliomba Wizara kuwekeza katika mchezo wa riadha kuwa kuwa ndio mchezo pekee unaoweza kuitangaza na kuajiri vijana wengi kwa wakati mmoja kuliko mchezo mwingine.
Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Harrison Mwakyembe alipongeza uongozi wa RT kwa juhudi zao na kuhaidi kutafuta dawa suala la ukame wa pesa hasa wanapoandaa mashindano makubwa kama hayo.
Pia alisisitiza njia yakusaka wanariadha kutumia michezo ya shule ni bora zaidi na kuwataka wanariadha kuwa na nidhamu pamoja na kufanya mazoezi kwa juhudi ndio njia ya mafanikio katika jambo lolote mtu analofanya.