Mzimu wa Kagere waendelea kuwatesa mashabiki Gor Mahia

Nairobi. Kwa zaidi ya siku mbili sasa tangu straika wao, Mnyarwanda Meddie Kagere aamua kugura Klabu ya Gor Mahia na kutimkia kwenye Simba SC, mashabiki wa klabu hiyo, wanaendelea kuweweseka kinoma!

Kagere aliyeitumikia Kogalo kwa misimu miwili ya mafanikio, alitua jijini Dar es salaam, siku ya Jumapili na Jumanne alisaini mkataba wa miaka miwili ya kuwatumikia mabingwa hao watetezi wa Ligi Kuu Tanzania Bara.

Mshambuliaji huyo aliyeipatia Gor Mahia ubingwa wa Sportpesa Super Cup, alikubali kutua katika mitaa ya Msimbazi, kwa dau la dola 50,000 (Ksh 10,000), mshahara wa dola 5,000 (Ksh 500,000) kwa mwezi, nyumba na usafiri wa kutanua nao mjini.

Hio sio 'ishu', habari kubwa kwa sasa ni hasira za mashabiki wa Gor Mahia. Unaambiwa jamaa wamechukia na wanamwona msaliti. Unakumbuka hasira za mashabiki wa Yanga dhidi ya Haruna Niyonzima alipoamua kuhamia Simba.

Sasa hasira za jeshi la kijani linaloongozwa na Jaro Soja, ni mara mbili yake. Wakionyesha kutokuamini, mashabiki Fredrick Oluoch, Eric Oyier, William Otieno na Camilla Lyn, kwa nyakati tofauti, waliposti kwenye ukurasa wao wa mtandao wa Twitter, wakisema kuondoka kwa straika huyo ni pigo kwa klabu

hiyo inayokabiliwa na mechi nyingi ikiwemo kutetea ubingwa wa ligi kuu.