Viporo vya Simba vya mtia hofu Julio

Dodoma. Kocha Jamhuri Kihwelu ‘Julio’ amesema Simba ilifanya kosa kusogeza mbele mechi zake kwa ajili ya kujiandaa na mchezo wa marudiano na Al Masry.

Simba imeondolewa katika mashindano ya Kombe la Shirikisho Afrika baada ya kulazimisha suluhu na Al Masry ugenini  na sasa tumaini lake pekee la kucheza mashindano ya kimataifa ni kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu Bara.

Julio alitaka viongozi wa Simba wasilichukulie poa ni suala la kuomba bodi ya ligi kusogeza mbele mechi zao za ligi kisa mechi za kimataifa ambapo kocha huyo mwenye mananeo mengi alisema jambo hilo linahatarisha uwezekano wa timu kuchukua ubingwa walioukosa kwa miaka mitano mfululizo sasa.

Julio anadai kuwa kusogezwa kwa mechi yao dhidi ya Njombe Mji iliyopaswa kuchezwa kabla ya kwenda Misri ilikuwa inawezekana kuchezwa ndipo wajiandae na safari ya kuwafuata Al Masry kama walivyofanya wenzao Yanga ambao baada ya kushinda wamewafikia idadi ya alama na kuongeza presha kubwa kwao.

“Hili walilolifanya viongozi wa Simba sikuona umuhimu wake na inahatarisha uwezekano wa kutwa ubingwa kwani walishawahi kulazimisha mechi zao kusimama hadi Yanga wakacheza viporo vyao baadaye Simba walipoanza kucheza mechi zao wakapata matokeo mabaya na kuwaruhusu Yanga kuchukua ubingwa,”alisisitiza Julio.

Kihwelu Julio alisema Simba haikuwa na bahati katika mechi zote mbili dhidi ya Al Masry jambo lililosababisha  timu hiyo kuondolewa bila kufungwa katika mechi zote mbili hivyo liwe funzo kwa wakati mwingine kuhakikisha wanapata ushindi nyumbani.

“Bahati haikuwa kwao Simba ukiangalia mechi ya kwanza nyumbani walicheza vema dakika za mwisho na pengine wangeshinda ila mvua ikawaharibia mwishoni matokeo yake wametolewa bila kufungwa na Waarabu hivyo wakati mwingine wahakikishe wanashinda nyumbani bila kujali ushindi wa aina gani,”alisema Julio.