Azam yamkuna Pluijm

Muktasari:

Azam imefuzu kucheza fainali ya Kombe la Mapinduzi na itacheza dhidi ya URA ya Uganda usiku wa leo, Jumamosi

 THOBIAS SEBASTIAN

Zanzibar. KOCHA wa Singida United Hans Van Pluijm ameisifia Azam katika mashindano hayo kuanzia nje ya uwanja mpaka ndani ambapo leo Jumamosi majira ya saa mbili usiku watacheza mechi ya fainali dhidi ya URA kwenye Uwanja wa Amaan, Zanzibar.

Pluijm alisema Azam wameonesha kuwa wapo makini kwani wamekuja huku Unguja wakitumia basi lao kwa kubebea wachezaji ni tofauti na timu nyingine zote ambazo zilikuwa zinatumia magari madogo (Haice) ambayo wakifatiwa na kamati ya mashindano.

"Katika mazingira ya kawaida kuwaweka wachezaji tofauti na wenzao unawajenga kifikra na kujiona wapo mazingira salama hivyo ndio Azam wameweza kufanya nje ya uwanja, " alisema.

"Jambo hilo linaweza kuongeza morali ya kushindana kwa wachezaji wakiwa uwanjani ni rahisi kupata matokeo ya ushindi ingawa mpira ni mchezo wa makosa, " alisema.

"Kiukweli katika mashindano hayo Azam wanastahili kufanya vizuri na hata walipofika hapo walistahili na nawapa nafasi ya kushinda na kuwa mabingwa katika mechi ya fainali, " alisema Pluijm.