‘Sikuja Simba kuleta maajabu’

Dar es Salaam. Kocha msaidizi wa Simba, Djuma Masoud amesema sikuja kufanya maajabu bali kusaidia ili timu isonge mbele na kuendelea kuwa namba moja kwenye msimamo wa Ligi Kuu Bara.

Kocha huyo Mrundi Masous alitambulishwa leo Simba kuchukua mikoba ya Mganda Jackson Mayanja aliejiondoa kuinoa timu hiyo kwa matatizo ya kifamilia.

Kocha huyo mwenye miaka 40, amekiri yeye ni mpole kiasi na pia mkali kwani huwa hapendi mtu achezee kazi yake kwani anachotaka  kutafuta riziki na timu isonge mbele.

"Siwezi kuahidi kuwa nitafanya nini  kwani kila kitu anapanga Mungu hivyo namuomba aniwezeshe kutumia ujuzi wangu pamoja na ushirikiano na kocha mkuu kuifanya Simba iwe ya kwanza mpaka ubingwa,” alisema msaidizi huyo wa kocha Joseph Omog.

"Sijaja kuleta maajabu ila nimekuja kusaidia kitu kidogo ambacho Mungu amenipa ili timu isonge mbele," alisema kocha huyo wa zamani wa Rayon Sports ya Rwanda.

Alisema yeye kuja kuwa kocha msaidizi Tanzania si jambo la kushangaza kwani Simba ni  klabu kubwa na anaitumia kama  shule ya kuzidi kusonga mbele.

"Watu wanaweza kushangaa Rwanda nilikuwa kocha mkuu na huku nimekuja kuwa msadizi, lakini wajue wakati nilianza nilianza chini na baadae nikasema nataka kupanda hivyo nikawa kocha mkuu, lakini Simba ni kama nimekuja kusoma kwani ni moja ya klabu kubwa hivyo kitu  kikubwa nataka nisogee mbele"alisema.

Naye Afisa Habari wa Simba, Haji Manara amewataka mashabiki na wanachama wa klabu hiyo kumpa ushirikiano kocha huyo.

"Kocha huyu anachukua nafasi ua Mayanja ambaye matatizo ya familia ndio yamemuondoa Simba na si kingine. Muda mrefu Mayanja alituambia juu ya matatizo yake na tukamuomba atuvumilie hadi tutakapomalizana na kocha mwingine ndipo aondoke," alisema Manara.
Pia, Manara alimtambulisha meneja mpya wa klabu hiyo, Richard Robert ambaye anachukua nafasi ya Cosmas Kapinga aliyerejea kwa mwajiri wake kuendelea na kazi yake ya udaktari.

Wasifu wa kocha:

Djuma Masoud (alizaliwa Agosti 30, 1977) amezichezea klabu za Prince Louis (2002), Rayon Sport (2003-2009) na Inter Star (2010).