Hesabu za Mbelgiji ni noma

Muktasari:

  • Ndanda itaikaribisha Simba, huku wakiwa na kazi ya kuzuia kasi za washambuliaji wa Simba, Meddie Kagere na Emmanuel Okwi ambao spidi yao imezidi kuongezeka kadri siku zinavyokwenda mbele.

MBELGIJI wa Simba, Kocha Patrick Asseums mjanja sana, kwani amekaa chini na kukuna kichwa kabla ya kupata njia mbadala ya kwenda kutumia katika uwanja wa Nangwanda Sijaona mjini Mtwara watakapokutana na Ndanda FC, kesho Jumamosi ili kuhakikisha anatoka na ushindi katika mchezo huo.

Ndanda itaikaribisha Simba, huku wakiwa na kazi ya kuzuia kasi za washambuliaji wa Simba, Meddie Kagere na Emmanuel Okwi ambao spidi yao imezidi kuongezeka kadri siku zinavyokwenda mbele.

Katika mazoezi ya mwisho waliyofanya kwenye Uwanja wa Boko Veterani, jijini Dar es Salaam kabla asubuhi ya jana hawajapanda mwewe na kwenda Mtwara, Mbelgiji alikuwa akitumia mbinu za kupita pembeni akitumia mawinga na mabeki wa pembeni.

Mabeki Mohammed Hussein ‘Tshabalala’ na Shomari Kapombe walikuwa wakitumika katika kupeleka mashambulizi huku wakisimamiwa kwa umakini wasiwe wazito katika kupiga krosi.

Katika mazoezi hayo njia ya krosi ndio ilikuwa ikitumika sana kwani washambuliaji wao John Bocco, Emmanuel Okwi, Meddie Kagere na Mohammed Rashid walikuwa wakitumia urefu wao vizuri katika kufunga.

Katika upande wa Mabeki aliwaweka Pascal Wawa, Paul Bukaba na Yusuph Mlipili ambapo Bukaba alionekana kumkosha Mbelgiji kwa namna ambavyo alikuwa akicheza na Wawa.

Viungo aliwapanga Erasto Nyoni, James Kotei na Mohammed Ibrahim ambaye alikuwa akipokezana na Said Ndemla, hata hivyo Ndemla nae alionekana kumkosha Mzungu huyo wakati huo huo Kapombe na Tshabalala wao wakitumika kama mawinga wa kupeleka mashambulizi.

Katika upande wa ushambuliaji aliwaweka Okwi na Kagere lakini njia waliyokuwa wanatumia kupokea mashambulizi mara kwa mara ni kupitia mipira ya krosi.

DILUNGA, MZAMIRU HAKISOMEKI

Wachezaji Mzamiru Yassin, Hassan Dilunga na kipa, Ally Salum wakati wachezaji wenzao wakiendelea na mazoezi, wao walikuwa wamekaa pembeni wakipewa programu maalum baada ya kupata majeraha.

Dilunga alionekana kupewa matibabu ya goti pamoja na kigundo cha mguu pamoja na Mzamiru, huku kipa Ally Salum aliyeshtua mkono wake nae akijumuishwa katika programu hiyo.

Programu waliyokuwa wamepewa ni kuzunguka uwanja kwa kutembea huku kila raundi wanayoenda wakitakiwa kupunguza mwendo na muda mwingine kuongeza ili waweze kupona majeraha yao polepole.

Wakati huo huo, kiungo Jonas Mkude alishindwa kufanya mazoezi na wenzake baada ya kuwa na matatizo ya kifamilia huku Asante Kwasi akisumbuliwa na malaria.

MBELGIJI AFUNGUKA

Baada ya mazoezi kumalizika kocha Patrick Asseums, alifunguka ameamua kutumia njia ya mawinga kupenyeza mashambulizi baada ya kuambiwa anaenda kucheza katika uwanja wenye changamoto nyingi.

“Nahitaji kupata matokeo katika mchezo huu kwahiyo unapokuwa unaenda sehemu tofauti na uliyozoea.”