OLIVER ALBERT
BEKI wa Kati wa Yanga, Isaac Boakye amedai watatisha kwenye Ligi Kuu Bara msimu ujao kuliko Simba lakini akakiri Mussa Hassan Mgosi ni mchezaji mzuri.
Boakye alisema ushindani mkubwa kwenye kikosi chao unampa jeuri ya kuwa timu yao itafanya vizuri lakini akasema Mgosi anastahili kuchungwa sana kwenye ligi hiyo.
"Ushindani ni mzito sana kwenye timu yetu na hiyo inatupa jeuri ya kumfunga yeyote, Yanga ni timu kubwa na hata Simba pia natumaini ligi itakuwa nzuri sana,"alisema.
"Yule mshambuliaji wa Simba anavaa jezi namba 11 (Mgosi) ni hatari sana nilimuona wakati wa mechi ya Simba na Yanga, alipofunga mabao mawili siku ile, ni mjanja sana na anajua sana mpira.
"Namkubali muda wowote anastahili kuwa mikononi mwa beki imara ili asilete madhara na nafikiri alistahili kuwa mfungaji bora msimu uliopita," alisema beki huyo ambaye siku hiyo alikuwa jukwaani.
"Sijawaona Simba hivi karibuni lakini ni timu nzuri kwa jinsi nilivyowaona wakati wa mechi na Yanga, wana wachezaji mahiri, wanacheza vizuri na watatupa ushindani sana ila sisi tuko zaidi yao."
Beki huyo amesajiliwa kuchukua nafasi ya Wisdom Ndhlovu aliyetupiwa virago kwa madai ya kushuka kiwango, lakini atakabiliana na upinzani mkubwa kutoka kwa Bakari Mbegu na Job Ibrahim.
Yanga tayari imeshaanza kambi kujiandaa na ligi itakayoanza Agosti 21, lakini wiki moja kabla watacheza mechi ya Ngao ya Hisani na mahasimu wao Simba kwenye Uwanja wa Taifa.