MICHAEL MOMBURI
KASHESHE ya kusaka namba ndani ya Azam inaumiza vichwa wachezaji, lakini kocha Itamar Amorin amecheka na kusema alisajili wachezaji wengi kusudi ili wapambane uwanjani.
Hali imekuwa pevu kwenye mazoezi ya Azam hasa nafasi za ushambuliaji na kiungo ambako kila nafasi ina wachezaji zaidi ya watatu wenye uwezo mkubwa.
"Unajua ukiwa na wachezaji wengi bora inasaidia kuwa na wigo mkubwa wa kuchagua kuliko kutokuwa nao, hali ya ushindani ambayo baadhi ya wachezaji wanazungumzia niliiweka kusudi,"alisema Itamar kocha wa zamani wa viungo wa Taifa Stars.
"Ukiangalia kwa mfano kwenye ushambuliaji kuna mchezaji kama Mrisho Ngassa, Peter Senyonjo, Kalimagonga `Kally' Ongala, Philip Arlando, John Boko hao ni baadhi tu wapo kama saba ambao wote wanawania namba mbili tu uwanjani.
"Kwenye kiungo ni hivyo pia, hali hali naifurahia nataka timu imara ambayo italeta mabadiliko msimu ujao, kiujumla kila nafasi uwanjani ina wachezaji watatu wazuri ndio maana ninaamini mambo yakienda vizuri, watu watafurahi ligi hii,"alisisitiza kocha huyo aliyedai bado anazisoma Yanga na Simba ingawa hajaziona.
Mshambuliaji Alando alisema: "Hali ni ngumu, ushindani ni wa kiwango cha juu kuliko watu wanavyofikiria na mbaya zaidi kila mtu ana uwezo na anataka kucheza, sijui nini kitatokea ngoja ligi ianze tuone mpangilio wa kocha ukoje, maana saa nyingine itategemea na mfumo anaotaka kutumia."
Azam imemsajili beki kisiki ambaye pia ni nahodha wa APR ya Rwanda, Patrick Mafisango, ambaye ameahidi vikombe msimu ujao.