OLIVER ALBERT
MAME Niang alichomoa bao dakika ya 87 na kuiepusha Kongsvinger na kipigo cha nne mfululizo kutoka kwa Tromso katika mchezo wa Ligi Kuu Norway uliochezwa juzi Jumapili.
Timu hiyo ambayo anaichezea kiungo wa Taifa Stars, Henry Joseph Shindika imekuwa haifanyi vizuri tangu kuanza kwa ligi hiyo na mashabiki wameitabiria kushuka daraja.
Tromso ndio walikuwa wa kwanza kupachika bao dakika ya 27 lililozamishwa na Bobbie Fribergda na kipindi cha pili baadae Henry ambaye anacheza kama beki wa kati katika timu hiyo alitolewa baada ya kushindwa kuonyesha kiwango kutokana na maumivu ya enka.
"Tutakaa sawa tu ingawa hali ni mbaya kwetu lakini nafikiri tunahitaji kuongeza nguvu katika kikosi chetu ili tuweze kufanya vizuri," alisema Henry.
"Ukiangalia timu yetu, wachezaji wengi wana umri mkubwa na kocha ameliona hilo na hapa tunachoomba tubaki kwenye ligi ili kocha asajili yosso," alijipa moyo Joseph, ambaye alikwenda Norway akitokea Simba.
Kongsvinger inashika nafasi ya 15 kati ya timu 16 zinazoshiriki ligi hiyo ikiwa na pointi 12 baada ya kucheza mechi 18, imefungwa 12, imeshinda tatu na imetoka sare mara tatu.
Rosenborg ndio inaongoza ligi hiyo ikiwa na pointi 40 baada ya kushinda mechi 11 na kutoa sare saba.