LOS ANGELES, Marekani
WIKI mbili zilizopita Lindsay Lohan alikataliwa kuingia katika klabu moja ya usiku iitwayo, Les Deux bila kuambiwa chochote, marafiki zake aliongozana nao waliruhusiwa kuingia.
Mwishoni mwa wiki hii akiwa na rafiki zake wengine walienda katika klabu nyingine ya usiku iitwayo, Voyeur nako alikataliwa na rafiki zake waliruhusiwa kuingia.
Baada ya kuzungumza nao kwa muda, mabaunsa wanaolinda klabu hiyo walimchukua mwanamuziki huyo na kumuingiza kupitia mlango wa nyuma.
Baada ya habari zake kuzagaa kwenye vyombo vya habari, Lohan amesema amegundua kuwa huo ni mchezo unachezwa kati ya mapaparazi na walinzi wa klabu hizo.
"Najua mapaparazi wanawalipa walinzi wafanya vile ili wao wanipige picha, nimeshaujua mchezo wenu tafuteni kingine cha kuandika kwani hamtanipata tena," alisema Lohan.
T Pain aja na Injili
"HUWEZI amini lakini ukweli ni kwamba huwa naenda kanisani mara nyingi kama ninavyoenda kwenye majumba ya starehe," anasema T Pain wakati akifanya mahojiano kuhusiana na ujio wa albamu yake mpya.
T Pain alisema ameshaimba sana nyimbo za kuufurahisha ulimwengu na sasa imebaki kuimba nyimbo za utukufu na kwamba albamu yake mpya itakuwa na nyimbo za Injili tupu.
Aliongeza kuwa wimbo wake wa kwanza kutoka ambao utakuwa wa utangulizi utaitwa 'Blame It On The Altar Wine'. Alisema albamu yake itaitwa Revolver.
"Nimeamua kufanya mapinduzi kwenye muziki wangu, nina albamu nne zote zinasifia na kuburudisha mambo ya ulimwengu tu, si kuwa nilimsahau aliyetuumba lakini nafikiri umefika muda wake wa kumpa sifa zote," alisema T Pain.