YANGA imefuzu Kombe la Shirikisho mwakani lakini Mrisho Ngassa hajaridhika na amesema fainali yake ni dhidi ya Simba, Aprili 11 kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Mchezaji huyo wa timu ya taifa mwenye mabao 12 ya kufunga sawa na John Boko 'Adebayor' wa Azam ameiambia Mwanaspoti kuwa kwake kazi bado kabisa.
Ngassa, ambaye huvaa jezi namba 16 akiwa na Yanga, amesema ana kazi kubwa ya kusaka kiatu cha dhahabu lakini pia fainali ya ligi msimu huu ni baina yao na Simba.
"Tumeshapata nafasi ya Kombe la Shirikisho lakini kwangu mimi bado ligi haijaisha bado kuna mechi na Simba inakuja ambayo naichukulia kama fainali ya ligi na hakuna masihara," alisema Ngassa, ambaye ni mtoto wa mchezaji wa zamani wa Simba na Pamba, Khalfan Ngassa.
"Hiyo mechi ndio naisubiri ni muhimu sana kwetu kwa vile tumekosa ubingwa kwa hiyo itatulazimu kuishinda au kupata matokeo mengine ya aina yoyote lakini si kupoteza.
"Tunataka kumaliza msimu vizuri na kuendeleza rekodi yetu," alisisitiza mchezaji huyo tegemeo kwenye kikosi cha kwanza cha Kocha Mserbia Kosta Papic.
Simba inahitaji kushinda mechi ijayo Machi 16 dhidi ya Azam ili kufikisha pointi 56 na kukabidhiwa kombe lake kwa kishindo lakini Yanga imeshafuzu Kombe la Shirikisho baada ya kuifunga Azam mabao 2-1 na kutimiza pointi 45 ambazo haziwezi kufikiwa na timu zilizoko chini yake.
Katika mzunguko wa kwanza ligi Simba iliifunga Yanga bao 1-0 lililofungwa na Mussa Mgosi lakini zilipokutana tena kwenye robo fainali ya Tusker, Yanga ikashinda mabao 2-1.