Mfadhili wa Yanga,Yusuf Manji akijadiliana jambo na Katibu Mkuu wa klabu hiyo,Lawrence Mwalusako. Manji amekaa na kocha Kosta Papic na kumaliza tofauti zao na kocha huyo kutangaza kwamba kila kitu kimekuwa sawa.
DORIS MALIYAGA
KATIBU Mkuu wa Chama cha Makocha Tanzania (Tafca) Eugen Mwasamaki amemwambia kipa wa JKT Ruvu, Jackson Chove kuwa:"Wewe ni Tanzania One, lakini jiamini zaidi."
Chove, ambaye pia yupo kwenye kikosi cha timu ya taifa 'Taifa Stars', ameonyesha kiwango cha juu katika mechi zote alizodaka na alipingia kipindi cha pili na kupangua penalti ya
Mussa Hassan 'Mgosi' baada ya Shaaban Dihile kuumia lakini ndani ya dakika sita za nyongeza, aliruhusu mabao mawili na kufanya matokeo kuwa 3-1 kwenye mechi kati ya timu hizo mbili, Jumamosi iliyopita.
Akizungumza na Mwanaspoti jana Jumatatu, Mwasamaki alisema, kiujumla Chove anazo sifa zote za kuwa kipa bora lakini alionyesha upungufu kwenye dakika za nyongeza zilizoongezwa kwenye mechi ya Ligi Kuu na Simba.
Alisema:"Tunaye kipa ambaye ni mzuri na huenda atatusaidia baadaye, lakini ana tatizo moja tu la kubabaika."
"Nina uhakika mabao yale mawili yaliyowapa ushindi Simba alikuwa na uwezo wa kuyazuia, lakini hali hiyo ya kutojiamini ilimwaribia," alieleza Mwasamaki.
Kwa upande wake, Chove alieleza changamoto kwake ni kujifunza kutokana na makosa lakini akajitetea bao la tatu lililofungwa na Uhuru Selemani lilikuwa la kuotea.