MASHABIKI wa Afrika Mashariki wamegeuzia macho yao kwa Simba ya Tanzania katika Kombe la Shirikisho baada ya timu zote za nchi tano zinazounda jumuiya hiyo kung'olewa kibabe katika michuano ya Shirikisho la Soka Afrika (CAF).
Simba ndio timu pekee ya nchi hizo iliyopangwa na CAF kuanzia raundi ya kwanza na sasa itaivaa Lengthens ya Zimbabwe kati ya Machi 19-21 jijini Harare, Zimbabwe.
Klabu zilizoenguliwa kwenye hatua ya awali ni Villa ya Uganda ambayo ilijitoa yenyewe, AFC Leopard ya Kenya iliyopigwa mabao 4-3 na Banks ya Ethiopia huku Miembeni ya Zanzibar ambayo ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikipigwa 4-2 na Petrojet ya Misri.
Atraco ya Rwanda ilitolewa kwa penalti 9-10 na Amal ya Sudan baada ya kufungana mabao 2-2, huku Atletico Olympic ya Burundi ikichapwa mabao 2-1 na Warri Wolves ya Nigeria.
Simba inajinoa vilivyo kwenye kambi yake ya mazoezi Bamba Beach jijini Dar es Salaam, huku kocha Patrick Phiri akisisitiza kuwa wanapiga hesabu za mbali katika michuano hiyo na wanajua mashindano yatakuwa magumu.
Endapo Simba ikiitoa Lengthens ya Zimbabwe kwenye mechi ya marudiano Aprili 4 jijini Dar es Salaam watacheza na mshindi kati ya Banks ya Ethiopia au Haras El Hodood ya Misri Aprili 23-25.
Katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika, ukanda huu umebakiwa na APR ya Rwanda tu ambayo inavaana na mabingwa watetezi, TP Mazembe ya Congo Machi 21 jijini Kigali huku mashabiki wengi jijini Kinshasa wakiitabiria maafa timu hiyo ya jeshi.
Simba ndio timu yenye rekodi nzuri kwa klabu za Tanzania kwenye michuano ya klabu barani Afrika kutokana na kufika nusu fainali ya Klabu Bingwa Afrika mwaka 1974, fainali ya Kombe la CAF (1993) na ilifuzu kwa hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika (2003).