MWANAMUZIKI Lil Wayne, ametengeneza video nane kwa kipindi cha mwezi mmoja huku akisubiri kusikiliza hukumu yake, na inakadiriwa huenda akafungwa kwa mwaka mmoja jela.
Mwanamuziki huyo alifikishwa mahakamani kwa mara ya kwanza Julai, 2007 kwa kosa la kukutwa na silaha kinyume cha sheria na baada ya uchunguzi yakinifu, Lil Wayne alipatikana na hatia.
Na sasa mwanamuziki huyo anafahamu ataingia jela ndio maana ameamua kutoa video kadhaa, ambazo zitaendelea kutamba wakati akiwa 'lupango'.
Mwanamuziki huyo ameshirikiana na "Diddy" Combs, Rick Ross, Drake na Travis McCoy katika kukamilisha video hizo.
Lil Wayne amesema ana mpango wa kuachia albamu mpya itakayokwenda kwa jina la 'Tha Carter IV' mwanzoni mwa mwaka 2011.
Na katika hatua nyingine, hukumu ya mwanamuziki huyo iliyokuwa itolewe katikati ya wiki hii iliahirishwa baada ya kutokea kwa moto katika Mahakama ya New York.
Jaji Charles H. Solomon alikuwa akisubiriwa kutoa hukumu lakini mtafaruku wa moto ulimfanya aahirishe. Tarehe nyingine ya hukumu hiyo haijatangazwa.