MPACHIKA mabao wa Tottenham, Jermain Defoe amewataka wanasoka watulie na kuacha kufanya mambo ya ajabu, ambayo yanawavunjia heshima.
Mshambuliaji huyo amesema wakati umefika kwa wachezaji wa England kujichunguza tabia zao na kuachana na baadhi ya mambo yasiyofaa.
Defoe amesema kuwa wanasoka wanatakiwa kuonyesha heshima ndani na nje ya uwanja.
Defoe mwenye miaka, 27 aliongeza: "Wachezaji wanapaswa kufahamu kwamba wao ni kioo cha jamii. Ni jambo rahisi kwa mtoto wadogo kujifunza tabia mbaya za mchezaji fulani kwa kuwa anampenda mwanasoka husika.
"Ni kweli hata sisi ni binadamu wa kawaida, ambao tunaweza kufanya makosa, lakini tunatakiwa kuachana na makosa yanayoepukika.
"Wachezaji wanatakiwa kuwa makini kwa kuwa katika kipindi hiki cha kuelekea fainali za Kombe la Dunia baadhi ya vyombo vya habari huibua skendo na kuwakosesha amani.
"Inakuwa ni vigumu kwa mchezaji mwenye kashfa kufanya vema katika fainali hizo hasa anapokutwa na skendo za ajabu," alisema.
Defoe pia alisema kuwa huwa hanywi pombe wala hajawahi kutumia dawa za kulevya.
"Tangu nikiwa mdogo nimekuwa nikijituma katika mazoezi na mama yangu amekuwa akiniambia kwamba nidhamu ndio mbinu pekee ya mafanikio."