Na Mwandishi Wetu
KOCHA Mreno Humberto Coelho aliyekuwa akiinoa Tunisia iliyoshindwa kufuzu fainali za Kombe la Dunia nchini Afrika Kusini ameomba kazi ya kuinoa na kuitengeneza upya Taifa Stars anayochezea Mrisho Ngassa na Mussa Hassan Mgosi.
Mreno huyo alisitishiwa mkataba wake baada ya kushindwa kuipeleka timu hiyo Afrika Kusini na mikoba yake kukabidhiwa Faouzi Benzarti ambaye ni kocha wa Esperance ya huko.
Coelho alijizolea sifa ulimwenguni mwaka 2000 baada ya kuiongoza Ureno iliyokuwa imesheheni vipaji kama winga wa zamani wa Barcelona na Real Madrid, Luis Figo, Rui Costa na Nuno Gomez kufika nusu fainali ya Euro 2000, ingawa baadae aliamua kubwaga manyanga.
Habari toka ndani ya Shirikisho la Soka la Tanzania(TFF) zilisema jana kuwa Mreno huyo ni miongoni mwa makocha walioomba kazi hiyo hivi karibuni huku akitamba kuitengeneza upya Stars kama alivyoifanya Tunisia.
Habari zinasema kocha huyo ambaye hakuwepo Angola amejinadi kuifanya kazi hiyo ipasavyo endapo atakabidhiwa mikoba hiyo.
Ingawa hakuna kiongozi yoyote wa TFF aliyekuwa tayari kutoa ufafanuzi jana lakini makocha zaidi ya saba inadaiwa wameshatuma maombi ya kuchukua nafasi ya Marcio Maximo anayemaliza mkataba wake Juni.
Coelho ambaye aliinoa Tunisia miezi 17, alitimuliwa baada ya kufungwa bao 1-0 na Msumbiji mjini Maputo kwenye mechi ya kufuzu kombe la Dunia huku yeye akitoa sababu kwamba wachezaji wake walikuwa hawajazoea nyasi bandia.
Kocha huyo mwenye miaka 59, ameinoa Ureno 1997-2000 akatimkia Morocco alikofanya kazi mpaka 2002. Mwaka 2002-04 aliinoa Korea Kusini alikofukuzwa, 2005-2006 alikuwa bosi wa Al-Shabab na kuanzia 2008 mpaka 2009 Tunisia.