Mwandishi Wetu
UONGOZI wa timu ya Yanga umesema kuwa unamuunga mkono kwa asilimia 100 kocha mkuu wa timu hiyo, Kostadin Papic katika suala zima la kuhakikisha kila mchezaji wa timu hiyo anazingatia majukumu yake ipasavyo pindi anapokuwa uwanjani ikiwa ni pamoja na nidhamu lengo ni kuhakikisha timu hiyo inafaya vizuri.
Hivi karibuni katika mazoezi ya timu hiyo, Papic aliwataka wachezaji wa timu hiyo kuhakikisha wanazingatia taratibu na maadili ya soka ikiwa ni pamoja na suala zima la nidham ili kuhakikisha wanafanya vizuri katika michezo yao yote ya Ligi Kuu iliyobakia.
Akizungumza na Mwananchi, Afisa Habari wa timu hiyo, Luis Sendeu alisema kuwa jambo hilo ni zuri na linalositahili hivyo uongozi wa timu hiyo upo bega kwa bega na kocha huyo kwa kila jambo ambalo linalenga katika kuleta mafanikio ndani timu hiyo.
"Ni kweli kabisa tunakabiliwa na mechi ngumu ambazo zinahitaji umakini mkubwa, ili tuweze kufanya vizuri katika mechi hizo inabidi wachezaji kuzingatia majukumu yao ipasavyo lakini wachezaji wanapokuwa wakifanya mzaha mazoezini, hata katika mechi wanaweze kufanya hivyo.
"Kwa pamoja tutashirikiana na kocha ili kuhakikisha kila mchezaji anazingatia majukumu yake ili kuhakikisha tunafanya vizuri katika mechi zetu zote za Ligi Kuu pamoja na katika mashindano ya kimataifa yaliyopo mbele yetu," alisema Sendeu.