LONDON, England
KIPA wa zamani wa Arsenal, David Seaman amemuacha mke wake wa pili ikiwa ni miaka 15 tangu alipoachana na mkewe wa kwanza.
Kipa huyo wa zamani wa England, ambaye alipewa jina la 'Mikono Salama' amewashangaza marafiki na ndugu zake kwa uamuzi huo.
Wikiendi hii, mke wa pili aliyeachwa aitwaye Debbie, ambaye ni mama wa watoto wawili (msichana na mvulana) alisema: "Kila mtu amechanganyikiwa lakini nina watoto wawili wazuri wa kuwalinda."
Mwaka 1994 gazeti la 'News of the World' liligundua kwamba Seaman ambaye sasa ana miaka 45, alimtelekeza mke aitwaye Sandra na watoto baada ya kuishi naye kwa miaka 10.
Ilielezwa kwamba mchezaji huyo wa zamani wa Arsenal alikimbia nyumba yake na kumuacha mkewe na watoto wawili Daniel na Tommy, wakati huo wakiwa na umri wa miaka saba na nane.
Waandishi wa gazeti hilo walimnasa mchezaji huyo akiondoka nyumbani kwake London kwa siri akiwa na mabegi mawili. Msemaji wa Seaman alisema kuwa kwa mara nyingine ameikimbia familia yake.
Alisema: "David ameikimbia familia yake kwa mara nyingine wiki chache zilizopita, tumejaribu kuweka mambo sawa lakini tumeshindwa, mawakili wanaoshughulikia talaka bado hawajaitwa lakini ndio kitu kinachofuata."
Rafiki yake wa karibu alisema: " Suala hilo ni kama kipindi cha nyuma wakati alipomtelekeza Sandra, hatukufahamu kama anaweza kurudia kitendo hicho lakini amerudia."