Wala msimpakazie Bi Mwenda jamani

Muktasari:

  • Bi Mwenda ambaye alianza kuvuma miaka ya 1990, alisema umahiri huo ndio umempa umaarufu, ingawa anakiri kuna wakati hupata wakati mgumu kwa watu kudhani yeye ni mchawi kweli.

KAMA unadhani yale maigizo ya kichawi anayofanya Bi Mwenda, kuna ukweli wowote wa kujua taaluma hiyo, utafeli. Mwigizaji huyo ambaye majina yake kamili ni Fatuma Makongoro, amefunguka kwa kusema kuwa hajui uchawi bali ni umahiri wake katika uigizaji tu.

Bi Mwenda ambaye alianza kuvuma miaka ya 1990, alisema umahiri huo ndio umempa umaarufu, ingawa anakiri kuna wakati hupata wakati mgumu kwa watu kudhani yeye ni mchawi kweli.

“Mimi sijui kabisa mambo ya uchawi wala ushirikina ni kazi tu ambazo lengo lake ni kufundisha jamii kupitia filamu, japo kuna wakati unaona hata watoto wanakuogopa na hata watu wazima wananichukulia sivyo kabisa,” alisema Bi. Mwenda.

Alisema hana roho mbaya kama vile uonekana katika baadhi ya kazi zake, pale anapocheza kama mama mkorofi asiyeweza kuishi na mkwe au mtu yeyote, ila anafanya vile kufikisha ujumbe kwa jamii juu ya watu wa aina hiyo.