Kwa Mama Mjatta ni nidhamu tu

Muktasari:

Amefichua kwamba, kama wasanii watahimiza na kukomalia nidhamu kwenye kazi basi watafika mbali na kuwa wasanii wakubwa ndani ya nje ya nchi.

MWIGIZAJI mkongwe nchini, Tecla Mjatta amefichua kuwa moja ya mambo yanayoweza kumsaidia msanii na kufika mbali ni kuzingatia nidhamu tu.

Amefichua kwamba, kama wasanii watahimiza na kukomalia nidhamu kwenye kazi basi watafika mbali na kuwa wasanii wakubwa ndani ya nje ya nchi.

Mama Mjatta alisema hata yeye hiyo ndiyo silaha yake kubwa na ndio maana licha kuwa katika sanaa kwa muda mrefu, hajawahi kuzungumzwa vibaya na watayarishaji kwa vile anazingatia sana suala zima la nidhamu kazini.

“Uigizaji ni kazi kama nyingine, nidhamu ni kinga kubwa kwa sanaa kwani miaka mingi tunaigiza, lakini ni nadra kusikia matukio yanayowagawa mashabiki wa kazi zetu, kwa kuwa tupo makini sana,” alisema.

Mwigizaji huyo ni mmoja ya wakongwe waliosalia kwenye sanaa ya uigizaji akiwa ameanza tangu enzi za Shirika la Filamu Tanzania (TFC) na amekuwa akiwakimbiza chipukizi waliopo sasa kwa kushiriki kazi nyingi na kushiriki matangazo ya biashara, ambayo yanawapa mkwanja mrefu.