Kha! Mangi ajishtukia, aruka kesi

MWIGIZAJI na msaili wa waigizaji wa filamu nchini, Abdul Ally ‘Mangi’ kama amejishtukia vile baada ya kukanusha tuhuma dhidi yake juu ya kudaiwa ana tabia ya kuwataka kimapenzi wasanii wa kike wanaosaka kazi kupitia kwake.

Mangi alisema tuhuma hizo zimekuwa zikimnyima raha, ilihali katika ufanisi wake wa kazi anazingatia misingi na maadili na kusisitiza hajui wanaompakazia wana nia gani dhidi yake.

“Kwa sasa kuna tatizo kubwa moja kila msanii chipukizi anaamini kuhusu skendo, anaweza kutokea msichana akaamua tu kusema Mangi ana tabia mbaya bila kujua ananiharibia,” alisema Mangi.

Mangi alisema hana tabia ya kuwataka wasanii rushwa ya ngono au wao kuonyesha viashiria vya mambo hayo, akiamini kufanya hivyo sio tu itamharibia, ila inaweza kuleta shida wakati wa malipo na kuwashauri wasichana kutojirahisisha.