Aunt Ezekiel, Iyobo waacheni tu

Muktasari:

Kauli hiyo ya mashabiki imetokana na tabia inayoonekana kuzoeleka ambapo nyota huyo hupenda kumvalisha mwanaye huyo mavazi yanayoonyesha mapaja.

KUTOKANA na alichokisema nyota wa filamu za Kibongo, Aunt Ezekiel, kuwa anapiga picha zinazoonyesha baadhi ya maungo yake kwa sababu za kibiashara, baadhi ya mashabiki wake wamemjia juu na kumtaka mambo hayo yawe yake tu na asimhusishe mwanaye.

Kauli hiyo ya mashabiki imetokana na tabia inayoonekana kuzoeleka ambapo nyota huyo hupenda kumvalisha mwanaye huyo mavazi yanayoonyesha mapaja.

Aunt na mzazi mwenzake, Moses Iyobo, wamekuwa wakipigiwa kelele na mashabiki wao katika mitandao ya kijamii kuwa wasipende kumvalisha mtoto wao huyo mavazi ya aina hiyo kwani si maadili ya Kitanzania na hayamjengei mtoto wao taswira nzuri mbele ya jamii.

Lakini Mwanaspoti lilipozungumza na Aunt Ezekiel kumuuliza kwanini anapenda kupingana na wanaomshauri kuhusu mavazi ya mwanaye huyo, akaamua kufunguka, tena kwa kutema shombo.

“Mimi ni mzazi mwenye akili timamu, najielewa nini nafanya. Majibu yangu mabaya kwa watu hutokana na wao kutumia lugha chafu katika ushauri wanaoutoa, sipendi lugha chafu. Inakera hadi kutupa hasira sisi wazazi,” alisema.

“Halafu kingine, kwanini watu wamekuwa mabingwa wakushauri familia za watu kuhusu malezi? Kwanza sioni kama namvalisha hizo nguo wanazodai hazina maadili. Watu wamezoea kusema tu kila kitu wanachokiona.”