Aah! Diamond na Zari acheni hizo bana

Muktasari:

  • Nyota huyo wa muziki wa kizazi kipya baada ya kuziona hizo picha alizichukua kama zilivyo na kuziposti katika ukurasa wake wa Inastagram na kuandika, ‘Ndiyo maana wakati mwingine naonaga bora tu nile na kusepa…maana hawathaminikagi wala kuaminika hawa’.

BAADA ya mrembo Zari Hassan ‘Zari the boss Lady’ wiki hii kuonekana akiogelea na mwanamume mmoja ambaye haijajulikana ni nani, unaambiwa Diamond ni kama alipagawa.

Nyota huyo wa muziki wa kizazi kipya baada ya kuziona hizo picha alizichukua kama zilivyo na kuziposti katika ukurasa wake wa Inastagram na kuandika, ‘Ndiyo maana wakati mwingine naonaga bora tu nile na kusepa…maana hawathaminikagi wala kuaminika hawa’.

Kauli hiyo iliibua maneno maneno katika ukurasa huo hadi Diamond akaamua kuichomoa picha hiyo lakini wakati huo huo Zari nae akaposti kwa kutoa maelezo ya kuwa yule ni binamu wa aliyekuwa marehemu mume wake Ivan, huku akitoa kauli za kashfa kwa wale wote waliokuwa wamamtolea maneno ya kashfa.

Hata hivyo, baada ya saa tano kupita, Diamond alitupia video akiwa na Zari pamoja na mtoto wao wa pili Nillan huku akiambatanisha na wimbo wa taarabu unaoitwa ‘Sitaki ushambenga’ ulioimbwa na mtoto wa Khadija Kopa, marehemu anaitwa Omari Kopa.

Wimbo huo ambao baadhi ya maneno yanasema mtu akiwa na mpenzi wake hawataki ushambenga wakigombana asubuhi jioni wanaongea hivyo watu hawawezi kuvunja penzi lao.

Posti hiyo ni kama ilichochea moto kwani mashabiki walianza kuwashambulia Diamond na Zari kwa kuwaambia walitaka kiki huku wengine wakisema labda Diamond anataka kutoa wimbo maana akitakaga kutoa wimbo huwa anajifanya kama amegombana na Zari ili watu waweke akili zao kwake.