Zitto Kabwe ajitosa urais TFF

Muktasari:

Habari za uhakika zinasema kwamba kiongozi huyo wa ACT-Wazalendo anayeheshimika miongoni mwa wanasiasa vijana nchini, ameshawishiwa na vigogo wa Simba pamoja na wanasiasa wengine wapenda michezo na ameonyesha nia ya dhati.

UCHAGUZI Mkuu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) unafanyika mwezi Agosti, lakini Mwanaspoti limehakikishiwa kwamba mwanasiasa machachari na shabiki wa kulia machozi wa Simba, Zitto Kabwe atawania urais.

Habari za uhakika zinasema kwamba kiongozi huyo wa ACT-Wazalendo anayeheshimika miongoni mwa wanasiasa vijana nchini, ameshawishiwa na vigogo wa Simba pamoja na wanasiasa wengine wapenda michezo na ameonyesha nia ya dhati.

Zitto kama atavaa viatu hivyo itakuwa ni mtihani kwa Jamal Malinzi ambaye bado haijafahamika kama atakitetea kiti chake ama la ingawa upepo unaonyesha hana dalili ya kubanduka.

Habari kutoka kwa mtu wa karibu wa Zitto ambaye Mwanaspoti halina wasiwasi nae, amedokeza kuwa Zitto anakitamani kiti hicho cha urais kwa nia ya kutaka kuleta mapinduzi katika soka la Tanzania na amepata jeuri zaidi kutokana na nguvu iliyoko nyuma yake. Zitto mwenyewe alipotafutwa hakupatikana kutoa ufafanuzi.

Mmoja ya vigogo hao ni Ismail Aden Rage, ambaye mara alipodokezwa taarifa hizo za Zitto aliyewahi kuwa Mjumbe wa Kamati ya Kamati ya Fedha katika uongozi wake, aliyesema haoni tatizo kwa mwanasiasa huyo kujitosa TFF.

Rage alisema anaamini Zitto ataleta mapinduzi na kila mpenda mabadiliko katika soka la Tanzania, lazima ajiunge pamoja naye kumuunga mkono Zitto na kwenda mbali kwa kusema atajisikia fahari kama atashinda kiti hicho.

“Nitafurahia akishinda Urais wa TFF kwa sababu atakuwa ameweka rekodi katika soka la Tanzania, kwa Mwanasimba kuwa Rais wa TFF kwani kwa miaka mingi, nafasi hiyo ya juu imekuwa ikishindwa na watu wa mtaa wa pili,” alisema.

Katibu Mkuu wa zamani wa TFF na klabu ya Simba, Michael Wambura alipoulizwa juu ya taarifa hizo za Zitto kutaka kujitosa urais wa TFF, alikataa kusema chochote.

Mkutano Mkuu wa TFF utafanyika Agosti 12 mwaka huu na moja ya ajenda kuu ya mkutano huo ni Uchaguzi Mkuu wa Shirikisho hilo ili kuchagua viongozi wa nafasi za urais, Makamu wake na Wajumbe wa Kamati ya Utendaji.