Wema, TID wajisalimisha, Vanessa Tundaman nao wamo!

Muktasari:

Mastaa hao pamoja na Mr Blue, Recho na Chid Benz walitajwa katika orodha ya wanaotuhumiwa na ‘unga’ iliyotangazwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda ambaye aliwataka wajisalimishe wenyewe polisi.

WAKATI Wema Sepetu na wasanii wa muziki wa kizazi kipya nchini, TID, Dogo Hamidu na mtangazaji, Babu wa Kitaa wakijisalimisha Polisi kuitikia wito wa kuhusishwa na Dawa za Kulevya, Vanessa Mdee naye ameunganishiwa kesi.

Mastaa hao pamoja na Mr Blue, Recho na Chid Benz walitajwa katika orodha ya wanaotuhumiwa na ‘unga’ iliyotangazwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda ambaye aliwataka wajisalimishe wenyewe polisi.

Jana Ijumaa asubuhi mastaa hao wanne walijisalimisha kwa hiari yao Kituo Kikuu cha Polisi, Dar es Salaam, ili kuhojiwa kabla ya mkuu wa mkoa huo naye kutinga kituoni hapo akiwa na orodha nyingine ya watuhumiwa wapya.

Katika orodha hiyo mpya ya Makonda iliyomtaja Vee Money, ina jumla ya watuhumiwa sita akiwamo Tundaman, Halidali Kavila, Amani, Kashozi na mfanyabiashara Omary Sanga anayedaiwa kusababisha asilimia 60 ya Watanzania kufungwa katika nchi za China na Hong Kong.