Mzambia Yanga amzidi akili Pluijm

Muktasari:

·Kocha huyo alichukua mikoba ya Pluijm Novemba mwaka jana wakati huo Yanga ikiwa katika nafasi ya pili na pointi 33, lakini akafanikiwa kukusanya pointi 35 katika duru la pili hivyo kumpiku Mzungu huyo.

KOCHA wa Yanga, George Lwandamina, amethibitisha kwamba ni kocha wa kiwango cha juu baada ya kuweka rekodi mbili kubwa ambazo zilimshinda mtangulizi wake Mdachi, Hans Van Pluijm.

Lwandamina ambaye ni raia wa Zambia, bado hajaaminiwa sana na watu wa Yanga, lakini rekodi zinaonyesha kwamba amefanikiwa kupiku idadi ya pointi 33 zilizokuwa zimekusanywa na Pluijm katika duru la kwanza huku akiweka rekodi ya kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu Bara baada ya kukaa nchini kwa miezi sita tu.

Kocha huyo alichukua mikoba ya Pluijm Novemba mwaka jana wakati huo Yanga ikiwa katika nafasi ya pili na pointi 33, lakini akafanikiwa kukusanya pointi 35 katika duru la pili hivyo kumpiku Mzungu huyo.

Yanga ikiwa chini ya Lwandamina, imepata pointi hizo mbili zaidi lakini bado ina mchezo mmoja mkononi ambao kama itashinda itakuwa imevuka kwa tofauti ya pointi tano.

Rekodi ya pili ya Lwandamina ni ya kutwaa ubingwa katika miezi sita ya kazi tu Jangwani jambo ambalo lilimshinda Pluijm katika msimu wake wa kwanza mwaka 2013/14 ambapo aliishuhudia Azam ikitwaa taji hilo mbele yake.

Kocha mwenye rekodi ya kutwaa ubingwa kwa miezi sita tu nchini ni Joseph Omog ambaye alitwaa taji hilo na Azam mwaka 2014 ikiwa ni miezi sita tu tangu alipopewa ajira hiyo.

MZUNGU AMBANA

Mbali na kwamba Lwandamina ameweka rekodi hiyo, bado anabanwa na rekodi mbalimbali za Pluijm ikiwemo ya kupata ushindi mkubwa zaidi na kuiwezesha timu hiyo kufunga mabao mengi zaidi.

Katika duru la kwanza Pluijm aliongoza Yanga kufunga mabao 31 ambayo Lwandamina ameshindwa kuyafikia kwani katika duru la pili timu hiyo imefunga mabao 26 tu.

Pluijm pia alipata ushindi mkubwa wa mabao 6-2 dhidi ya Kagera Sugar katika duru la kwanza rekodi ambayo imeshindwa kufikiwa na Lwandamina ambaye ushindi wake mkubwa zaidi ni wa mabao 4-0 dhidi ya Stand United na Ndanda.

WACHEZAJI HEWA

Wakati Yanga ikisubiri kuthibitishwa bingwa mpya wikiendi hii, wachezaji wanne watavaa medali kupitia migongo ya wenzao kwani wamekuwa na mchango mdogo.

Nao ni mabeki Pato Ngonyani na Oscar Joshua na mastraika butu Matteo Antony na Malimi Busungu.