Mashabiki Yanga waonywa

Dar es Salaam. Shirikisho la soka Tanzania (TFF) limewaonya mashabiki wa soka nchini hasa wa klabu ya Yanga, kutofanya vitendo vyovyote vya utovu wa nidhamu katika mechi zitakazochezwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na waandishi wa habari leo, Afisa Habari wa TFF, Alfred Lucas alisema kuwa shirikisho limebaini mikakati ya baadhi ya mashabiki hasa wa klabu ya Yanga, kujipanga kufanya vitendo vinavyoashiria kueneza chuki na kashfa kwa viongozi wa serikali na TFF kwenye mchezo wa ligi ya mabingwa Afrika kesho dhidi ya Ngaya Club De Mbe ya Comoro na ule wa Ligi Kuu dhidi ya Simba, Februari 25.

"Shirikisho limebaini mkakati wa mashabiki kuingia uwanjani na mabango ya kuwatusi na kuwadhalilisha viongozi wa serikali na wa shirikisho hivyo tunawaonya mashabiki hao wasifanye hivyo kwani iwapo wakibainika, watachukuliwa hatua kali za kisheria.


Mechi zote hizo zitafuatiliwa kwa ukaribu na viongozi wote wa serikali hivyo kama vitendo hivyo vitafanyika, basi huenda serikali ikachukua uamuzi mgumu ambao unaweza kugharimu mchezo wa soka," alisema Lucas.