Kiungo Godfrey Bony afariki

Mbeya. Kiungo wa zamani wa Yanga na Taifa Stars, Godfrey Bony amefariki usiku wa kuamkia leo katika Hospitali ya Makandani Wilaya Rungwe, Mbeya alipokuwa amelazwa.
Dada wa marehemu, Neema Bony amethibitisha kifo cha kaka yake aliyekuwa amelazwa hospitalini hapo wiki mbili zilizopita.
"Ni kweli ametutoka, ila nashindwa kutaja muda kamili aliyofariki kwani sisi (ndugu) jana usiku saa tatu tuliondoka hospitali baada ya kumhudumia, hivyo leo asubuhi tumekwenda kwa ajili ya kumumhudumia tumekuta amefariki.".
Amesema utaratibu wa hospitalini hapo hakuna ndugu anayeruhusiwa kulala na mgonjwa wodini, hivyo muda wote mgonjwa anakuwa chini ya uangalizi wa wauguzi wa zamu.
Amesema tangu alipofika hospitali alianza kupata nafuu lakini siku nne zilizopita alianza kubadilika hali yake.
"Muda huu ndugu wote wamerudi nyumbani kwa ajili kupanga taratibu za mazishi.
Katika uhai wake Bony 'Ndanje' amewahi kucheza kwa mafanikio katika timu za Tukuyu Stars, Tanzania Prisons, Yanga na baadaye kucheza soka la kulipwa nchini Indonesia.