Fedha za uchaguzi za TFF zaleta balaa

MABOSI TFF wameitaka Kamati ya Utendaji Chama cha Soka Arusha (ARFA), kupeleka ripoti ya fedha zilizotumika kwenye uchaguzi wa chama hicho.

Mjumbe wa Kamati ya Uchaguzi ya TFF, Jeremiah Wambura aliyekuwa mmoja wa waangalizi wa uchaguzi huo alisema TFF ilitoa Sh. 2 milioni ili kufanikisha uchaguzi huo.

Kabla uchaguzi kuanza, mgombea nafasi ya mwenyekiti,  Peter Temu alitaka kujua fedha hizo zilivyotumika hali iliyomshitua Wambura na kutoa agizo la kupata muhtasari.

“TFF wametoa Sh. 2 Milioni kwa ajili ya posho za wajumbe, nimeona wamepewa 35,000 tu, kwa hesabu za haraka hata milioni 1 haifiki, mtuambie zimetumikaje?” Alihoji Temu.

Mwenyekiti aliyemaliza muda ARFA, Khalifa Mgonja alisema hakupewa taarifa ya vipi fedha zitumike ingawa aliahidi kutoa taarifa kwa maandishi.