Mashabiki wa Yanga wakauka uwanjani

Muktasari:

Yanga ndiyo timu iliyotwaa ubingwa wa Ligi Kuu Bara mara nyingi zaidi 27


Dar es Salaam. Pamoja na Yanga kurudi kwa kasi katika mbio za ubingwa bado mechi zake zimeshindwa kuwavutia mashabiki wake.

Yanga imeshinda michezo yake saba ya Ligi Kuu bara, lakini aina ya kikosi chake kwa sasa imeshindwa kuwavutia mashabiki wa mabingwa hao mara 27.

Yanga iwapo itashinda mechi yake ya sasa dhidi ya Stand United ikiwa inaongoza kwa mabao 2-0 hadi dakika 27, itafikisha pointi 46, sawa na Simba wanaongoza Ligi Kuu Bara kabla ya kuingia kwenye mapumziko ya wiki mbili.

Yanga inayosifika kwa kuwa na mashabiki wengi nchini msimu huu imeshindwa kuvutia mashabiki wake na hata wale waliopo uwanjani wanaonekana kutokuwa na shamla shamla kama ilivyozoeleka.

Katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa kati ya Yanga na Township Rollers ya Botswana ni mashabiki 9,961 tu walioshudia mechi hiyo na kuingiza Sh 56.2 milioni.

Wakati watani zao Simba mechi yake ya Kombe la Shirikisho dhidi ya Al Masry uliofanyika usiku ulishudiwa na mashabiki 14,798 na kuingiza Sh 85 milioni.