Kumbe ndoa ya Mama Diamond iko hivi buana!

HABARI kubwa mjini ni Zari ‘Thebosslady’ kumbwaga baba watoto wake, Diamond Platinumz na umaarufu na mkwanja wake wote.

Diamond a.k.a Chibu alimwagwa siku ya Wapendanao (Valentine Day), ambapo mengi yamezungumzwa mpaka sasa lakini, jamaa amepiga kimya tu.

Baada ya Mwanaspoti kumsaka kwa muda na kupishana naye, limefanikiwa kumnasa mama yake Diamond, Sanura Kassim, ambaye ni maarufu zaidi kwa jina la Sandra.

Mama Diamond amefunguka mambo kadhaa kuhusu maisha yake na ya mwanaye huyo, ambaye anatamba sana.

Kama hukuwa unafahamu, Sandra alipata mateso makubwa kuwalea watoto wake, lakini sasa amekaa kivulini akila matunda, kwa kuwa maisha anayoishi kwa sasa, hayakuwepo akilini mwake miaka kadhaa iliyopita.

Historia yake na Diamond inaonyesha ni watu waliopitia maisha ya shida, manyanyaso na karaha za kila namna. Ni mama, ambaye amechangia kiasi kikubwa kumpa sapoti mwanae, Diamond katika suala la muziki, kwani mojawapo ya simulizi yake anasema, alikuwa akienda naye kwenye matamasha ya muziki enzi hizo na hata kudiriki kumwombea ili apate nafasi ya kuimba jukwaani.

Chukua muda wako kidogo usome mahojiano ya Mwanaspoti na Sandra, ambaye hivi karibuni ilitangazwa kuwa aliolewa tena.

Mwasapoti: Shikamoo mama.

Mama Diamond: Marhaba, nani mwenzangu.

Mwanaspoti: Natokea Mwanaspoti na naomba tuzungumze mawili matatu kuhusu ndoa yako pamoja na sakata la mkwe wako Zari kuandika katika mtandao wa kijamii kuwa ameamua kuachana na mwanao kipenzi, Diamond.

Mama Diamond: Ohoo! umeanza na wewe, nilijua tu utaniuliza kuhusu Zari, haya anza maswali yako.

Mwanaspoti: Asante mama. Hivi ni kweli umeolewa au ni habari tu za mitandaoni?

Mama Diamond: Ni kweli nimeolewa, tena nimeolewa na mwanaume yule yule waliyekuwa wakisema katika mitandao kuwa ni mdogo. Ila nawashangaa angekuwa mdogo angeoa.

Na ndoa ilikuwa kimya sababu, tumeshakuwa watu wazima na ndoa sio Promo (matangazo) useme umtangazie kila mtu japo watu wengi tu walihudhuria. Sema sio wale mliokuwa mnawataka nyinyi waliozooleka kuhudhuria kila ndoa za watu.

Mwanaspoti: Baada ya kufunga ndoa nini matarajio yenu?

Mama Diamond: Kuongeza familia.

Mwanaspoti: Kuna tetesi kuwa wewe ni mjamzito?

Mama Diamond: Ujauzito ni jambo la kheri, kama ipo itatokeza tu, nyie nihesabieni miezi tu.

Mwanaspoti: Diamond amechukuliaje kushuhudia ukiolewa, akiwa na umri mkubwa?

Mama Diamond: Amechukulia kawaida tu, tena amefurahi sana.

Mwanaspoti: Kwa upande wa Baba Diamond, vipi hakuleta shida yoyote kwa kuolewa kwako?

Mama Diamond: Kwa sasa kila mtu na maisha yake, ataletaje shida mtu miaka kibao siko naye jamani!

Mwanaspoti: Kuna ukweli wowote wa Zari kuachana na Diamond?

Mama Diamond: Kiukweli swali hili ungempata Zari au Diamond ndio wangekujibu vizuri, sifahamu hilo.

Mwanaspoti: Inasemekana kuwa Zari ameamua kuachana na Diamond baada ya kipande cha video kilichoonyesha Diamond na Wema wakiwa karibu na pia kuhusu suala lake na Hamisa, baada ya kukubali kumlea mtoto aliyezaa naye.

Mama Diamond: Bwana eeh mie nimechoka maswali, mbona humalizi tu? Nishakwambia sijui hayo mambo watafute wenyewe, mbona unataka niongee vitu nje ya uwezo wangu?

Mwanaspoti: Ile posti ya Zari katika Instagram kuhusu kumuacha Diamond uliiona?

Mama Diamond: Nimeiona.

Mwanaspoti: Umeichukuliaje ile posti?

Mama Diamond: Nimeichukulia posti imetumwa na mkwe wangu, ambaye amenizalia watoto, Tifah na Nilan.

Mwanaspoti: Watu wanasema kwa sasa spidi ya vijembe katika Instagram imepungua kutokana na Zari kutoa tamko la kuachana na Diamond?

Mama Diamond: Mie huwa siposti vijembe, sema watu huwa wanatafsiri tofauti na ukiona kimya sijaposti kitu ujue dokta natafuta dawa.

Mwanaspoti: Inasemekana una bifu na Hamisa Mobeto?

Mama Diamond: Hapana sio kweli, achana na habari za mitandaoni.

Mwanaspoti: Toka Hamisa ajifungue, hujawahi kuposti mtoto wake kama unavyowaposti watoto wa Zari, kwanini?

Mama Diamond: Nitamposti tu wala usijali kwani yule ni mjukuu wangu, kwanini nisimposti? Sema watu wanataka watakavyo sio nitakavyo.

Mwanaspoti: Kuna habari kuwa una tabia ya kuwa bendera kufuata upepo, yaani mwanao Diamond akiwa na mwanamke huyu nawe unahamia huko, akiwa na mwingine vivyo hivyo na pia kumchagulia mwanamke. Hili likoje?

Mama Diamond: Mie nishazoea kuambiwa hivyo, ila watu watambue Diamond ni mtu mzima ana uwezo wa kuchagua mwanamke anayemtaka yeye na sio kuchaguliwa. Kuhusu hilo la kuwa mimi ni bendera wache tu waniambie hivyo, tena sio bendera tu hata mlingoti kwangu poa tu.

Mwanaspoti: Asante kwa ushirikiano mama.

Mama Diamond: Karibu tena.