Hazard katikati ya viburi viwili vya Perez

Muktasari:

Imeanza taratibu kule Madrid. Real Madrid inamtaka Eden Hazard. Ilianza taratibu kama hivi mwaka 2001 wakati Florentino Perez alipoitangazia dunia kwamba anamtaka Zinedine Zidane. Bosi wa Juventus, Luciano Moggi, alibisha.


PESA inaongea? Labda, lakini mara chache sana huwa inashindwa kuongea. Florentino Perez ana utajiri wa dola bilioni moja tu. Roman Abramovich, ana utajiri wa dola bilioni tisa. Wakati mwingine kiburi kinaongea kuliko pesa. Usishangae sana.

Imeanza taratibu kule Madrid. Real Madrid inamtaka Eden Hazard. Ilianza taratibu kama hivi mwaka 2001 wakati Florentino Perez alipoitangazia dunia kwamba anamtaka Zinedine Zidane. Bosi wa Juventus, Luciano Moggi, alibisha.

Waandishi wa habari walipomfuata Perez pale ofisini aliwapa jibu rahisi tu. “Hakuna kitu kisichouzwa duniani, inategemea una kiasi gani cha pesa”. Siku chache baadaye Zidane alitua Santiago Bernabeu akivalishwa jezi namba 5 ya Madrid na kutambulishwa kwa waandishi wa habari na mashabiki waliofurika.

Ilianzia hivyo hivyo mwaka 2008 wakati Perez alipotangaza kumtaka Cristiano Ronaldo. Alitumia njia za kimafia kidogo ambazo zilimuudhi Sir Alex Ferguson. Inasemekana alimlaghai Ronaldo nyuma ya mgongo wa Manchester United. Sir Alex alichukia kweli kweli. Akawaambia waandishi wa habari :“Siwezi kufanya biashara na lile genge la wahuni.”

Haikuwezekana. Julai 2009, Ronaldo alikuwa akitambulishwa mbele ya mashabiki 80,000 wa Real Madrid na kuvunja rekodi ya utambulisho aliyofanyiwa Diego Maradona na mashabiki wa Napoli miaka 25 kabla ya hapo ambapo Maradona alitambulishwa mbele ya mashabiki 75,000.

Hauwezi kubishana na Perez. Si bilionea kuliko Manchester United au Roman Abramovich. Hata hivyo, mashabiki wa Chelsea inabidi wawe na wasiwasi kwelikweli wanaposikia kuwa anamtaka Eden Hazard. Kama kweli anamtaka lazima atamchukua tu.

Uvumi unaanza kusambazwa makusudi katika gazeti maarufu la michezo la Hispania, Marca. Baada ya hapo uvumi unapelekwa kwa mwandishi mchambuzi maarufu wa soka la Hispania, Guillem Balague. Lengo kubwa linakuwa kumtia mchezaji mhusika katika presha na kumweka katika mkao wa kula.

Perez ana viburi viwili. Kwanza kabisa ana moyo wa kiuwendawazimu ambao matajiri wa klabu zote kubwa duniani hawana. Katika wachezaji 10 wa mwisho ambao wamevunja rekodi ya uhamisho wa dunia, Perez amevunja kwa wachezaji watano.

Perez anaweka pesa mezani ambazo Abramovich hajawahi kuweka kwa mwili wa mchezaji mmoja. Si kila tajiri ana uwezo wa kuwa na roho ya kiuwendawazimu kama ya Perez. Bei anayoweka mezani kwa ajili ya mchezaji mmoja inaweza kununua wachezaji watano bora.

Kiburi cha pili ambacho ni kikubwa zaidi ni historia ya Real Madrid. Hakuna mchezaji ambaye hataki kuichezea Real Madrid. Hili linaifanya kazi ya Perez na pesa zake iwe ndogo. Hazard nataka kucheza Real Madrid, Alexis Sanchez anataka kucheza Real Madrid, Paul Pogba yupo tayari hata kesho, Sergio Aguero, hata ukimuamsha usingizi atakwenda Santiago Bernabeu.

Kuna watu walifanya kazi ngumu huko nyuma ya kuifanya Madrid iwe klabu bora duniani. Wakongwe kina Ferenc Puskas. Kina Alfred de Stefano na wengineo. Madrid ndio klabu bora zaidi katika uso wa ulimwengu kwa mujibu wa takwimu na kila kitu.

Baadaye walipita kina Zidane, Figo, Ronaldo de Lima na wengineo. Matokeo yake imekuwa timu ya ndoto ya kila mwanasoka mwenye kipaji. Kila mmoja wao anataka kwenda kuacha nyayo zake Santiago Bernabeu. Ukijumlisha na kazi ya pesa za Perez, maisha yanakuwa rahisi zaidi kwa Madrid.

Bahati mbaya zaidi kwa Chelsea ni kwamba simwoni Galactico mwingine anayeweza kuwindwa na Perez zaidi ya Hazard. Sioni nafasi ya Neymar kwenda Madrid ukizingatia kuwa Barcelona inamwandaa kuwa Messi wao, lakini pia wamejifunza kutoka katika makosa waliyofanya kwa Luis Figo mwaka 2000.

Galactico aliyebaki sokoni, mwenye kipaji, haiba, mvuto na kila kitu anabakia kuwa Hazard. Lakini pia imepita miaka minne sasa tangu Perez alipoishtua dunia. Ni miaka minne sasa tangu Perez alipofanya ubabe. Manchester United imetia doa majivuno na ubabe wa Perez kwa kuvunja rekodi ya uhamisho msimu uliopita.

Kwa asili ya Madrid wakati mwingine inatangaza ubabe si tu kwa sababu ya uwezo wa mchezaji, hapana, bali ni katika kuidhihirishia dunia ukubwa wa klabu yao. Ni kama ilivyofanya kwa Gareth Bale. Hakuwa mchezaji aliyefanana na pesa alizosajiliwa, lakini Perez aliamua kuwakumbusha mashabiki tu ukubwa wa Santiago Bernabeu.

Nadhani Perez atarudi tena kuishtua dunia kidogo na kuirudisha Madrid juu ya Manchester United katika msimamo wa wavunja rekodi.

Ana sababu nyingi kwa Hazard, lakini kumbuka kuwa ifikapo Februari 5 mwakani, Ronaldo atakuwa anatimiza miaka 33. Hawezi kuendelea kuwa Ronaldo yule tunayempenda na kumfahamu.

Barcelona imejiandaa na uzee wa Messi. Wana Neymar ambaye ana miaka 25 tu.

Je, Madrid imejiandaa na uzee wa Ronaldo? Jibu linakuwa hili ambalo Perez analitafuta kwa sasa katika miguu ya Hazard. Mwisho wa siku hakuna kinachoshindikana kwake. Tusubiri kidogo.