Kocha Brazil aita 15 Kombe la Dunia

Muktasari:

  • Brazil ni bingwa mara tano wa Kombe la Dunia ikiwa ndiyo nchi iliyotwaa taji hilo mara nyingi zaidi

Rio de Janeiro, Brazil. Kocha wa Brazil, Tite ametaja majina ya wachezaji 15, wenye uhakika wa kuwepo katika kikosi kitakachokwenda Kombe la Dunia, Russia.

Tite amefanya kitu ambacho si kawaida wakati wa mahojiano na UOL Esporte, amekitaja kikosi hicho kikiwa na nyota wanne wa Paris Saint-Germain: Daniel Alves, Marquinhos, Thiago Silva na Neymar.

Kutoka katika Ligi Kuu England, mshambuliaji wa Liverpool, Roberto Firmino, kiungo wa Chelsea, Willian na nyota wawili wa Manchester City, Gabriel Jesus na Fernandinho.

Kiungo mpya wa Barcelona, Philippe Coutinho na Paulinho, kutoka Real Madrid wapo Casemiro na Marcelo, kipa wa Roma, Alisson, pia Miranda wa Inter Milan na Renato Augusto wa Beijing Guoan ni miongoni mwa wachezaji waliotaja.

Tite ameacha nafasi nane ambazo zitajazwa kutegemea na viwango vyao kwa beki wa Juventus, Alex Sandro na winga Douglas Costa pamoja na kipa  wa Manchester City, Ederson.

Kocha huyo alimaliza kwa kusema: "Orodha hiyo bado ipo wazi kwa mchezaji kuingia na kutoka pia."