Acheni uchuro nyie! Njombe haishuki daraja

Dar es Salaam. Mshambuliaji wa Njombe Mji, Ditram Nchimbi amesema licha ya kuwa kwenye nafasi ya  mwisho kwenye  msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara watahakikisha hawashuki daraja.

Katika michezo 17 ambayo Njombe Mji imecheza, imeshinda mara mbili, kufungwa mara nane na kutoka sare mara saba, jumla ya pointi walizokusanya ni 13.

“Mazingira tuliyopo kwenye msimamo sio mazuri, hivi karibuni tumekuwa na michezo migumu ambayo tulipanga kupata matokeo ya ushindi lakini ndiyo kama ilivyotokea.

“Bado tuna nafasi ya kupigana ili tujinasue kwenye hatari ya kushuka daraja, ndiyo kwanza tumeanza mzunguko wa kwanza hivyo tuna kila sababu ya kuanza kuyabadili matokeo mabaya  kuwa matokeo mazuri,” alisema mshambuliaji huyo wa zamani wa Mbeya City.

Njombe Mji ambayo mchezo wake uliopita ilipoteza mbele ya Yanga kwa mabao 4-0 itakutana na Simba, Februari 25 baada ya kucheza michezo yake miwili ya nyumbani kwenye uwanja wao wa Sabasaba dhidi ya Mbeya City na Majimaji.