Kesi ya Wema yapigwa kalenda
Muktasari:
Awali Wema alikiwa akitetewa na Peter Kibatala ambaye alijitoa.
Dar es Salaam. Shahidi wa pili wa Upande wa Mashtaka, Inspekta Wille ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa aliijaza fomu ya kupima sampuli ya mkojo wa Wema Sepetu ofini kwake kabla hajapimwa kwa Mkemia Mkuu wa Serikali.
Inspekta Wille, pia alidai kuwa hajawahi kupeleka sampuli za mkojo za washtakiwa Angelina Msigwa na Matrida Seleman Abbas ambao ni wafanyakazi wa Wema kwenda kuchunguzwa kwa Mkemia Mkuu wa Serikali kuhusu kukutwa na dawa za kuleAllyvya aina ya bangi.
Shahidi hiyo aliyaeleza hayo leo mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba wakati akihojiwa na Wakili wa upande wa utetezi, Albert Msando baada ya kutoka ushahidi wake.
Shahidi hiyo alidai kuwa aliijaza fomu ya kupeleka sampuli ya mkojo wa Wema saa nne kamili asubuhi akiwa ofini kwao na kuandika maneno mkojo ndani ya chupa ya plastiki.
Alidai kuwa aliijaza hivyo kwa sababu ya uzoefu kwa miaka 15 kuwa ukifika katika ofisi ya Mkemia mkuu wa Serikali mkojo unakuwa katika chupa ya plastiki.
Aliendelea kudai kuwa Februari 8,2017alifika katika ofisi za Mkemia Mkuu wa Serikali saa tano asubuhi na kumkabidhi Mchunguzi Elia Mulima kichupa cha plastiki ambacho ndani kilikuwa na mkojo.
Wakili Msando alimuuliza shahidi ulikuwapo wakati sampuli ya mkojo uliokuwamo ndani ya kichupa cha plastiki unaodaiwa kuwa ni wa Wema wakati unachukuliwa ambapo Inspekta Wille alidai kuwa hakuwapo.
Wakili Msando alimuuliza Inspekta Wills anaweza kusema kuwa unajua kwa uhakika kilichokuwa ndani ya chupa ya plastiki kuwa ni mkojo wa Wema. Baada ya kuulizwa hilo, Inspekta Wille alidai kuwa yeye hajui.
Msando alimuhoji Inspekta Wille kuwa walikaa kwa muda gani katika Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Inpekta Wille alidai kuwa hakumbuki.
Shahidi huyo alidai kuwa yeye hakupekuwa katika chupa anacholala Wema bali alipekuwa katika chumba anachohifadhia nguo ikiwamo nguo na viatu.
Alidai kuwa katika upekuzi walikuta msokoto wa bangi jikoni juu ya kabati, pia walikuta msokoto wa bangi uliotumika ukiwa ndani ya kiberiti dirishani katika chumba wanacholala wafanyakazi wa Wawili wa Wema.
Hata hivyo walishindwa kueleza msokoto huo ni wanani kati ya wafanyakazi hao wakili wa Wema.
Mahakama iliipokea hati ya ukamataji mali iliyojazwa katika upekuzi uliofanyika nyumbani kwa Mlimbwende wa Tanzania mwaka 2006 na msanii wa Filamu, Wema Sepetu kama kielelezo.
Kesi imeahirishwa hadi Februari 26 na 27, 2018 itakapoendelea kusikilizwa kwa ushahidi wa mashahidi wa upande wa mashtaka.
Inspekta Wille awali akitoa ushahidi wake kwenye kesi hiyo alidai katika upekuzi huo walifanikiwa kukuta misokoto inayodhaniwa kuwa ni dawa za kulevya aina ya bangi.
Kwa pamoja wanakabiliwa na mashtaka mawili ya kukutwa na kiwango kidogo cha dawa za kulevya na kutumia dawa za kulevya.
Wille alidai kuwa Februari 4, 2017 anaikumbuka kwa sababu aliitwa na Mkuu wake wa kazi na kupewa kazi ya kufanya upekuzi nyumbani kwa Wema na aliongozana na WP Mary, Koplo Robert, PC Hassan na dereva kuelekea Unonio anapoishi Wema ili wakaufanye upekuzi huo.
Inspekta Wille alidai kuwa walipofika nyumbani kwa Wema huko Ununio waligonga mlango na kwamba waliwakuta wasichana wawili ambao ni wafanyakazi wa Wema na wakaomba waitiwe mjumbe wa nyumba kumi Steven Noho wakaitiwa.
Shahidi huyo wa pili wa upande wa mashtaka alidai kuwa walimueleza kuwa wamekwenda nyumbani kwa Wema kwa nia ya kufanya upekuzi nyumbani kwa Wema na wanatafuta dawa za kulevya na kitu chochote ambacho wangekitilia shaka.
Wema alisema dada yake awepo ili ashuhudie upekuzi huo, dada yake alifika na tukapekuwa ambapo upekuzi wetu ulianzia jikoni ambapo juu ya kabati la vyombo tulifanikiwa kukuta msokoto mmoja unaodhaniwa kuwa ni bangi na karatasi ya kusokotea, Alieleza shahidi huyo wa pili wa upande wa mashtaka.
Katika chumba cha Wema ambacho anahifadhia nguo na vitu vyake vingine mlango ulikuwa umefungwa lakini wafanyakazi wake walituletea, tukafungua na tukafanikiwa kukuta vipisi na msokoto unaodhaniwa kuwa ni bangi dirishani.”Alieleza shahidi huyo wa pili wa upande wa mashtaka.
Akiendelea kutoa ushahidi kwenye kesi hiyo, Inspekta Wille alidai kuwa upekuzi huo uliendelea katika chumba cha wasichana wa kazi wa Wema, walifanikiwa kukuta kiberiti ambacho ndani yake kulikuwa na msokoto ambao unaonekana umeishavutwa.
Alidai kuwa baada ya kufanya upekuzi huo, walisaini hati ya ukamataji wa mali ambapo yeye aliisaini, Wema mwenye aliisaini, wafanyakazi wake, dada yake, pamoja na mjumbe wa eneo la Unonio.
Aliongeza kuwa baada ya hapo walienda kituoni na kumkabidhi mtunza vielelezo, Robert.
Inadaiwa kuwa Februari 4,2017 katika Makazi ya Wema huko Kunduchi Ununio washtakiwa hao walikutwa na msokoto mmoja na vipisi vya bangi vyenye uzito wa gramu 1.08.
Kwa upande wa Wema yeye anadaiwa kuwa Februani Mosi, 2017 katika eneo lisilojulikana jijini Dar es Salaam, alitumia dawa za kulevya aina ya Bangi.
Wema ni miongoni mwa watu waliotajwa na Mkuu wa Mkoa Dar es Salaam, Paul Makonda wakituhumiwa kujihusisha na dawa za kulevya.
Inadaiwa kuwa Februari 3, 2017, Wema alijipeleka mwenyewe katika Kituo cha Polisi Kati ambapo alikamatwa.